KAMPUNI ya Bia ya Tanzania (TBL) kwa kushirikiana na Kampuni ya Mawasiliano ya simu za mikononi ya Vodacom Tanzania amezindua mfumo wa malipo kwa wakulima uliopewa jina la BanQu.
Mfumo huo wa BanQu utawezesha shughuli zote za manunuzi na malipo kati ya TBL na wakulima kuwekwa kwenye kumbukumbu na kurahisisha ufuatiliaji na uhakiki kwa pande zote mbili kwa njia ya kidigitali. Anaripoti Faki Sosi …(endelea).
Akizindua mfumo huo leo tarehe 31 Mei, 2022 jijini Dar es Salaam, Waziri Habari, Mawasiliano na Teknolojia ya Habari, Nape Nnauye amesema Serikali inaunga mkono jitihada hizo zitakazoinua sekta ya kilimo nchini.
Amesema mfumo huo utawezesha sekta ya kilimo kukua kwa kutengeza mfumo wezeshi kwa wakulima kwenye kulifikia soko.
“Sekta hii inagusa maendeleo ya mtu mmoja mmoja na baadaye Taifa zima, ndio sekta inayowashughulisha Watanzania asilimia 70 mpaka 80” amesema na kuongeza kuwa.
“Vodacom kupitia M-Pesa imerahisisha mfumo wa kifedha kwa wakulima kwa kuwa huduma za benki hazipo vijijini ambapo wakulima hupatikana.
“Uamuzi wa Vodacom unakwenda kuwasaidia wakulima kwenye huduma za kifedha na kutawasaidia uchumi wa nchini yetu” amesema.
Mkurugenzi Mtendaji wa TBL, Jose Moran amesema teknolojia ya BanQu itawezesha wakulima kupata taarifa zitakazo wawezesha kulinda maslahi ya wakulima.
Amesema TBL imeweka mipango thabiti ya kuwanufaisha wakulima “Hivi sasa asilimia 74 ya malighafi inayotumiwa na TBL inatoka kwa wakulima wa ndani ya nchi”.
Aidha, Mkurugenzi wa Mawasiliano wa TBL, Mesia Mwangoka amesema mfumo huo tayari umesajili zaidi ya wakulima 6500 ambao TBL hununua mazao kwao, watalipwa kupitia M-Pesa na kuongeza kuongeza mnyororo wa thamani.
Naye Mkuregenzi Mkuu wa Vodacom, Sitholizwe Mdlalose amesema Vodacom kupitia mfumo wa BanQu imekusudia kuwainua wakulima ili wapate tija wakiwa shambani bila kusafiri umbali mrefu kutafuta huduma za kifedha.
Amesema huduma hiyo itaongeza thamani ya mazao yao kwa kuwa inapunguza mianya ya upotevu wa pesa unaotokana na kusubiri kwa muda mrefu au kutembea umbali mrefu kufuatilia malipo yao.
Wakati Mkurugenzi wa M-Pesa, Epimack Mbeteni amesemamfumo huo unakwenda kuwakomboa Watanzania kwa kuwa mtandao huo imejidhatiti kuwahudumia wananchi.
Leave a comment