MAMLAKA ya Usimamizi wa Wanyamapori Tanzania (TAWA) imetoa wito kwa wadau wa utalii kuwekeza katika maeneo ya vitalu 12 vya uwekezaji maalumu (SWICA) ambavyo mwekezaji atamiliki eneo hilo kwa miaka 30. Anaripoti Danson Kaijage, Dodoma … (endelea).
Wito huo umetolewa jana tarehe 3 Novemba, mwaka huu na Kaimu Kamishna ya Uhifadhi wa Mamlaka ya Wanyamapori nchini (TAWA), Mabula Misungwi katika kongamano la Kampuni za Uwindaji wa Kitalii nchini (TAHOA) lililofanyika jijini Arusha.
Kongamano hilo limelenga kutoa elimu ya uwekezaji mahiri katika maeneo hayo ya vitalu 12 vya uwekezaji maalumu (SWICA) yanayosimamiwa na TAWA.
Misungwi amesema TAWA imeandaa mkakati maalumu wa kuvutia wawekezaji mashuhuri duniani.
Amesema ili kupata fursa ya kuwekeza, kampuni ya mwekezaji mzawa itatakiwa kulipia dola za Marekani milioni 10, kampuni inayomilikiwa na mzawa na mgeni itatakiwa kulipia dola za Marekani milioni 20 wakati mgeni itatakiwa kuwa na mtaji wa dola za Marekani milioni 50.
Aidha, Afisa Mhifadhi – Kitengo cha Huduma za Biashara kutoka TAWA, Said Habibu amewaeleza washiriki wa kongamano hilo kuchangamkia fursa mbalimbali za uwekezaji zinazopatikana katika maeneo yanayosimamiwa na TAWA.
Ametaja maeneo ambayo yametengwa kwa uwekezaji ni Maswa Mbono, Maswa Kimani na Mkungunero.
Mengine ni pamoja na Ikorongo, Grumeti, Rungwa-Inyonga, Lake Natron (E), Selous LL1, Selous MT2, Selous Ml1, Selous MHN1 na Selous MH12
Katika kikao hicho wadau hao wamesema vikao hivyo vitasaidia kuboresha mambo mbalimbali hususani uwekezaji na uwindaji unaostahili.
Aidha, wadau hao wametoa pongezi kwa elimu hiyo waliyoipata na kuahidi kufanya kazi kwa ukaribu na TAWA.
Katika kikao hicho wadau hao wa utalii walitoa maoni mbalimbali ya namna ya kuboresha SWICA.
Kikao hicho kiliratibiwa na Taasisi ya Serikali inayosimamia sekta binafsi (TPSF) chini ya Mwenyekiti wake Angelina Ngalula.
Leave a comment