MAMLAKA ya Mawasiliano Tanzania ( TCRA) kwa kushirikiana na Jeshi la Polisi limemfikisha kwenye Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu, Fadhili Mahenge anayedaiwa kumiliki kadi za simu (Line) 626 alizokuwa akitumiwa kwa utapeli. Anaripoti Faki Sosi … (endelea).
Mbele ya Hakimu Mkazi, Wanjah Hamza, wakili wa Serikali Batilda Mushi amemosema shitaka la kwanza mtuhumiwa. Amedai kuwa ametenda kosa la kusambaza taarifa za uongo ambapo inadaiwa kwa siku tofauti kati ya mwezi Januari 2017 na Mach 2019 katika eneo la Dar es Salaam, Rukwa , Songwe na nje ya nchi alisambaza ujumbe wa ‘Tuma Pesa kwenye namba hizi’ akijua kuwa ujumbe huo ni wa uongo.
Shitaka la pili kuanzisha na kusambaza ujumbe bila ridhaa ya mpokeaji ambapo inadaiwa kuwa mtuhumiwa kwa siku tofauti kati ya mwezi Januari 2017 Machi 2019 eneo la Dar es Salaam, Rukwa, Songwe na sehemu nyingine nje na ndani nchi alianzisha na kusambaza jumbe kwa kutumia simu kadi (Line) 626 kutoka mitandao tofauti bila ridhaa ya wapokeaji jumbe hizo.
Kosa la tatu ni kujipatia fedha kwa njia ya udanganyifu ambapo mtuhumiwa anadaiwa kwa siku tofauti kati ya mwezi Januari 2017 na Machi 2019 katika eneo la Dar es Salaam, Rukwa, Songwe na nje ya nchi kwa makusudi na kwa nia ya kupotosha alijipatia fedha kupitia simu kadi (Line)626 zilizosajiliwa kwa majina yake alijipatia Sh. 123 milioni.
Kosa la tano ni utakatishaji Fedha ambapo inadaiwa kuwa mtuhumiwa anadaiwa kwa siku tofauti kati ya mwezi Januari 2017 na Machi 2019 katika eneo la Dar es Salaam, Rukwa, Songwe na nje ya nchi alitakatisha Sh. 123 milioni akijua kwamba fedha hiyo ni zao la kujipatia fedha kwa njia ya udanganyifu.
Wakili Batilda wakili amedai kuwa upepelezi haujakamilika. Wakati huo huo Wakili wa utetezi, alisema shitaka la tano limejielekeza kwenye utakatishaji fedha lakini linatokana na shitaka la nne mahakama ielekeze mshitakiwa kupewa dhamana.
Wakili Batilda akijibu hoja za upande wa utetezi amedai kuwa mtuhumiwa ameshitakiwa kwa hati ya uhujumu uchumi na utakatishaji fedha na ili tuyazungumzie ni lazima tupate hati ya ruhusa kutoka kwa Mkurugenzi wa Mashtaka (DPP).
“Ili kuwe na chaji ya ya utakatishaji fedha nimlazima kuwe na kosa lilizalisha kosa la utakatishaji fedha kwa hivyo haya makosa mawili tofauti.”
Hakimu Wanjah ametupilia mbali pingamizi la utetezi na kuihailisha kesi hiyo mpaka tarehe 2 Mei 2019.
Leave a comment