JESHI la Polisi, Kanda Maalum ya Dar es Salaam linamshikilia Halima Juma (23), Mkazi wa Chalinze kwa tuhuma za wizi wa fedha kupitia mashine za kutolea fedha (ATM). Anaripoti Hamis Mguta … (endelea).
SACP Lazaro Mambosasa, Kamanda wa Polisi wa Kanda hiyo amesema, Halima anashikiliwa mara baada ya kutiliwa shaka.
Amesema, tarehe 19 Novemba 2019 katika benki ya CRDB, tawi la Mbagala akiwa katika ATM, alitiliwa shaka baada ya kuingia kwenye chumba cha ATM ya benki hiyo akijifanya kuwasaidia wazee na wastaafu wasiojua kutumia mashine hizo.
“Lengo lake ni kuchukua namba za siri za wastaafu na wazee hao, kisha kuwabadilishia ATM kadi zao na baadaye kuwaibia fedha kwenye akaunti zao kwa kutumia kadi halisi za wahusika,” amesema na kuongeza;
“Mtuhumiwa huyo alikamatwa na askari wanaolinda Benki hiyo, na alipopekuliwa alikutwa na kadi 23 za watu mbalimbali za benki tofauti, zikiwa katika pochi yake huku akiwa amezificha katika sehemu zake za ukeni.”
Kamanda Mambosasa amewataka wastaafu kuwa makini na wizi wa aina hiyo, na kuhakikisha wanaongozana na watu wanaowaamini kwa msaada wa kutoa pesa katika mashine hizo.
Kadi alizokutwa nazo ni CRDB 07, NMB 06, NBC 02, AMANA 02, Pasta Benk 02, ACB 01, STANIBIC 01, DTB 01 na EQUITY 01.
Amesema, mtuhumiwa anaendelea kuhojiwa na atafikishwa mahakamani hivi karibuni.
Leave a comment