TANZANIA imetoa msaada wa kibinadamu kwa nchi za Zimbabwe, Malawi na Msumbiji, baada ya nchi hizo kukumbwa na maafa yaliyotokana na kimbunga cha Idai. Anaripoti Mwandishi Wetu … (endelea).
Msaada huo ambao ulikuwa pamoja na mahindi tani 200, mchele tani 14 na dawa za binadamu tani 24 ulikabidhiwa kwa mabalozi wa nchi hizo hapa nchini, na Waziri wa Mambo ya Nje, Profesa Palamagamba Kabudi na Waziri wa Afya, Ummy Mwalimu leo tarehe 19 Machi 2019 leo tarehe 19 Machi 2019, jijini Dar es Salaam.
Waziri Ummy na Kabudi walikabidhi misaada hiyo kwa niaba ya Rais John Magufuli, ambapo mara baada ya kukabidhiwa, misaada hiyo ilipakiwa kwenye ndege ya Jeshi la Wananchi kwa ajili ya kusafirishwa katika nchi hizo.
Akizungumza baada ya makabidhiano hayo, Prof. Kabudi amesema shida za majirani wa Tanzania ni za serikali kwa kuwa leo kwao kesho huenda ikawa kwetu, hivyo Tanzania ina wajibu wa kutoa msaada.
Prof. Kabudi ameyataka mashirika binafsi na kampuni nchini kutoa misaada ambayo itapokelewa na Ofisi ya Waziri Mkuu.
Waziri Ummy amesema baada ya kupewa maelekezo na Rais Magufuli ya kutoa msaada, waliwasiliana na mawaziri wa afya wa nchi ya Zimbabwe, Msumbiji na Malawi ili kupata mahitaji ya dawa, ndipo akaelezwa kwamba, nchi hizo zinahitaji dawa za kuzuia maambukizi ya bacteria na magonjwa ya matumbo.
Aidha, Waziri Ummy amesema serikali ya Tanzania iko tayari kutoa msaada katika sekta ya afya ikiwemo kutoa baadhi ya madaktari wake kwa ajili ya kusaidia wahanga katika nchini hizo.
Kimbunga cha Idai kilianzia nchini Zimbabwe usiku wa Alhamisi kisha kuhamia katika nchi za Msumbiji na Malawi, ambapo inasemekana kimepoteza maisha ya watu takribani 1,000 huku kadhaa wakikosa makazi sambamba na miundombinu kuharibiwa.
Leave a comment