SERIKALI ya Tanzania, imesisitiza miongozo yote iliyotolewa kwa umma kujikinga dhidi ya maambukizi ya Virusi vya corona (COVID – 19), izingatiwe. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dodoma … (endelea).
Mkurugenzi wa Idara ya Kinga wa wizara ya afya, maendeleo ya jamii, jinsia, wazee na watoto, Dk. Leonard Subi amesema, Tanzania ni salama.
Hata hivyo, Dk. Subi amesema, bado kuna tishio la maambukizi ya virusi hivyo duniani, ni muhimu kuendelea kuchukua tahadhari za kujikinga.
Dk. Subi amesema hayo leo Jumanne, tarehe 8 Juni 2021, alipohojiwa na moja ya chombo cha habari jijini Dodoma ni hatua gani Tanzania inaendelea kuzichukua kuhakikisha jamii inakingwa dhidi ya wimbi jipya la maambukizi ya COVID-19.
“Tanzania tupo salama, lakini tunatakiwa kuendelea kuchukua tahadhari dhidi ya maambukizi hayo ambayo kwa takriban mwaka na nusu sasa bado yanaikabili dunia.”
“Wizara kazi yetu ni kuendelea kihimiza wananchi kujikinga dhidi ya COVID -19, tuendelee kuchukua tahadhari,” amesema Dk. Subi.
“Tuliona katika wimbi la kwanza 2020 wananchi waliitika wito wa kunawa mikono, kuvaa barakoa, kukaa umbali, kufanya mazoezi, lishe bora na masuala mengineyo,” amesema.
Dk. Subi amesema, “tunataka kusisitiza kinachotokea Afrika maambukizi yanaongezeka na baadhi ya wakuu wa nchi wanatoa matamko kama tulivyomsikia Rais wa Uganda, Yoweri Mseven na sisi Tanzania tumekuwa na mwingiliano na uhusiano mwema na nchi jirani.
“Watanzania kinga ni bora kuliko tiba tusije tukasubiri kuingia kwenye mitungi ya oksijeni, tuendelee kujikinga. Hali ni shwari hata Rais Samia Suluhu Hassan, anachukua tahadhari kujikinga na maambukizi akikutana na watu mbalimbali,” amesema.
Mkurugenzi huyo amesema, “mashuleni, vituo vya afya tuliweka vifaa kwa kunawa kwa maji safi tiririka, tunawe mikono.”
Leave a comment