SERIKALI ya Tanzania imerejesha huduma ya safari za ndege za abira za kimataifa, zilizositishwa mwezi mmoja uliopita. Anaripoti Regina Mkonde, Dar es Salaam … (endelea).
Tanzania ilisitisha safari za nje tarehe 13 Aprili, 2020 kwa ajili ya kudhibiti maambukizi ya ugonjwa wa homa kali ya mapafu, inayosababishwa na virusi vya corona (Covid-19).
Jana Jumatatu, tarehe 18 Mei, 2020, kupitia ukurasa wake wa Twitter, Dk. Hassan Abbasi, Msemaji Mkuu wa Serikali ya Tanzania, amesema Tanzania imeondoa zuio la safari za ndege za abiria kutoka nje, ili kuruhusu shughuli za usafiri wa anga na utalii, kurejea kama ilivyokuwa zamani.
Wakati huo huo, Dk. Abbasi amesema Tanzania imeondoa zuio la kujiweka karantini kwa muda wa siku 14 kwa abiria wote wanaowasili nchini. Na kwamba, watapimwa Covid-19 pamoja na kukaguliwa taarifa zao za afya.
“Aidha, Serikali imeondoa zuio la kujitenga siku 14 kwa abiria wote wanaowasili nchini, wageni au wenyeji, badala yake kipimo cha kawaida kitafanyika na ukaguzi wa taarifa za kiafya wanakotoka ili kujiridhisha kuwa wanaowasili hawana maambukizi ya Corona,” amesema Dk. Abbas.
— Msemaji Mkuu wa Serikali (@TZMsemajiMkuu) May 19, 2020
Naye, Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, Isack Kamwelwe akizungumza jijini Dodoma jana Jumatatu, alitoa maagizo kwa Mamlaka ya Usafiri wa Anga Tanzania (TCAA), Mamlaka ya Viwanja vya Ndege Tanzania (TAA), Kampuni ya Kusimamia na kuendeleza Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Kilimanjaro (KADCO) na Shirika la Ndege Tanzania (ATCL) kuanza kutoa huduma bila kikwazo na kuzingatia taratibu za kiafya zilizotolewa na Shirika la Afya Ulimwenguni na Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Nchini.
Waziri Kamwelwe alisema ndege zote za kibiashara, misaada, kidiplomasia, dharura na ndege maalum zinaruhusiwa kuruka na kutua katika viwanja vyote nchini.
Hatua hiyo ya Tanzania kufungua anga lake la kimataifa, imechukuliwa siku moja baada ya Rais John Magufuli kueleza kwamba, kuna idadi kubwa ya watalii wanataka kuja kutalii nchini.
Rais Magufuli alitoa kauli hiyo Jumapili ya tarehe 17 Mei, 2020, aliposhiriki ibada katika Kanisa la Kiinjili la Kilutheri Tanzania (KKKT), Usharika wa Chato, mkoani Geita.
Pia, Rais Magufuli alisema anafikiria kufungua vyuo, endapo hali ya mwenendo wa maambukizi ya Covid-19, itaendelea kupungua kama ilivyo sasa.
Alisema idadi ya wgaonjwa waliopona Covid-19 nchini imeongezeka kwa kasi, huku maambukizi mapya yakipungua.
Leave a comment