TANZANIA imepunguza maambukizi ya ugonjwa wa Trachoma (vikope) kutoka wilaya 71 hadi sita ambazo zitaendelea na umezaji kingatiba. Anaripoti Hamis Mguta … (endelea).
Hayo yamesemwa leo na Mratibu wa Taifa wa Magonjwa yaliyokuwa hayapewi kipaumbele kutoka Wizara ya Afya Dk. Upendo Mwingira wakati wa mafunzo ya kimataifa ya uchukuaji wa takwimu za ugonjwa wa vikope yanayofanyika jijini Arusha.
Dk. Mwingira amesema kuwa nchi inajivunia kwa mafanikio makubwa kwani hivi sasa wilaya 65 hazihitaji tena kingatiba kulingana na vigezo vilivyowekwa na Shirika la Afya Duniani (WHO).
“Lengo la WHO hadi ifikapo mwaka 2020 tuwe tumeweza kutokomeza ugonjwa wa Trachoma kama tatizo la kijamii, kwamba hatutaki maambukizi mapya,” amesema.
Aidha, alisema mwaka 2010 katika tathimini Tanzania kulikua na makadirio ya wagonjwa 160,000 wa vikope lakini kutokana na jitihada za Wizara ya Afya hadi Julai 2018 inakadiriwa wagonjwa hao wamepungua mpaka kufikia 17,000.
Hata hivyo Dk. Mwingira amesema zoezi la kusawazisha vikope hapa nchini linaendelea zaidi ya mikoa kumi katika halmashauri zenye maambukizi.
Mafunzo hayo yanahusisha wataalam wa macho kutoka mataifa mbalimbali Duniani na kwa nchi za Afrika yanahudhuriwa na nchi za afrika Mashariki, Magharibi na Kati.
Leave a comment