WAKATI Tanzania ikielekea kwenye ujenzi wa uchumi wa kati, serikali imeonesha hofu juu ya kupungua kwa fedha za misaada kwa ajili ya miradi ya maendeleo, na mikopo yenye masharti nafuu. Anaripoti Dany Tibason, Dodoma … (endelea).
Hofu hiyo imeoneshwa na Dk. Phillip Mpango, Waziri wa Fedha na Mipango, wakati akizungumza na maafisa mipango wa wizara na idara za serikali, jijini Dodoma jana tarehe 20 Desemba 2019.
Akizungumza katika mkutano huo, amesema watu wengi wanatamani Tanzania iingie kwenye kundi la nchi zenye uchumi wa kati, lakini hatua hiyo, itapunguza misaada ya fedha za miradi ya maendeleo.
Dk. Mpango ameeleza zaidi kuwa, nchi zinazoingia kwenye uchumi wa kati, taasisi za fedha hasa Benki ya Maendeleo ya Afrika (AfDB) pamoja na Benki ya Dunia (WB), hupunguza utoaji wa mikopo yenye masharti nafuu, kwenye nchi husika.
“Najua wengi mnatamani tuingie kundi la nchi zenye uchumi wa kati, lakini mfahamu kwamba maana yake ni kuwa, baadhi ya vyanzo vya ugharamiaji wa miradi ya maendeleo ambavyo tulikuwa tunategemea, hususan misaada ya maendeleo na mikopo ya masharti nafuu, nayo itapungua, ” ameeleza Dk. Mpango na kuongeza;
“Mnafahamu baadhi ya mabenki tunayoitegemea, Benki ya Maendeleo ya Afrika, Benki ya Dunia, zote hizi wanafikiria Tanzania imekuwa na uchumi wa kati, maana yake kwa upande wa Benki ya Dunia hatutakuwa tunategemea mikopo ya gharama nafuu peke yake, lakini maana yake watataka tuchanganye mikopo ya gharama nafuu na yenye gharama kubwa zaidi.”
Serikali ya awamu ya tano chini ya Rais John Magufuli, inaendesha miradi mbalimbali ya maendeleo, ikiwemo miundombinu na kuhamasisha ujenzi wa viwanda, ili kuipelekea Tanzania kwenye uchumi wa kati.
Leave a comment