SERIKALI ya Tanzania, imepanga kupunguza gharama za hereni maalum ya utambuzi wa mifugo nchini ili kumpunguzia gharama mfugaji.
Kauli hiyo imetolewa leo tarehe 9 Septemba jijini Dodoma na Waziri Mkuu Kassim Majaliwa wakati akijibu swali la Mbunge wa Nkasi, Aida Khenani (Chadema).
Khenani aliuliza kuwa ni serikali ina mpango gani wa kupunguza gharama za upigaji chapa kwa mifugo ambayo ni Sh 1750 kwa ng’ombe mmoja lakini serikali isiwatoze wafugaji gharama mpya za hereni zinazopotea pindi mifugo hiyo ikiwa malishoni.
Akijibu swali hilo, Majaliwa alisema serikali itafanya tathmini ya bei ya ununuzi wa hereni hiyo inayobandikwa sikio kwa ng’ombe lakini pia wizara ya mifugo nayo itaandaa utaratibu kwa mfugao ambao umepoteza hereni urejeshewe hereni bila kutozwa pesa nyingine.
“Tumetafuta njia kadhaa, tumegundua kupiga chapa tunapoteza ubora wa ngozi, kwa mfano tulipoanza kutumia kiwanda cha Kilimanjaro ngozi hizo hazitumiki.
“Njia ya kutumia kuvalisha hereni, mwanzo tulikuwa tunatoboa lakini sasa tunabandika… inawezekana ng’ombe mmoja mmoja anadondosha hereni.
“Lakini katika kikao cha juzi, mjadala huo uliibuka na kukubaliana kuwa wizara wataondoa hizo tozo kwa mara ya pili. Kinachotakiwa ni taarifa za mfugo huyo kujazwa upya katika fomu ambayo ipo mtandaoni kisha kupatiwa hereni mpya,” alisema.
Leave a comment