SERIKALI imesema ina malengo ya kuongeza idadi ya watalii hadi kufikia 5,000,000 ifikapo 2025, ambao wataingiza fedha Dola za Marekani 6 bilioni. Anaripoti Regina Mkonde, Dar es Salaam … (endelea).
Hayo yameelezwa leo Jumamosi, tarehe 14 Januari 2023 na Waziri wa Maliasili na Utalii, Balozi Pindi Chana, akizungumza katika mkutano wa kueleza namna Serikali inavyosimamia na kuhifadhi wanyamapori Tanzania, uliofanyika mtandaoni ambao umeandaliwa na Taasisi ya Watch Tanzania.
“Tuna-target ya kufikia watalii wasiopungua takribani milioni 5 ifikapo 2025, lakini pato la takribani Dola za Marekani bilioni 6 ifikapo 2025. Hivi sasa pato kutoka Julai mpaka Desemba 2022 ilikuwa Sh. 186 bilioni na mtakumbuka mwaka jana tulikuwa tuna-recover kutoka COVID-19. Katika kipindi hicho Pato la Taifa limekwenda hadi Sh. 389 bilioni,” amesema Balozi Pindi.
Waziri huyo wa Maliasili na Utalii, amesema Serikali inatekeleza miradi mbalimbali kwa ajili ya kuongeza mapato yatokanayo na sekta hiyo, ikiwemo ujenzi wa viwanja vya ndege, kufungua utalii maeneo ya Kusini, kuendelea kuboresha hifadhi za taifa 22 na hifadhi za wanyamapori 33.
Aidha, amewataka wananchi kushirikiana na Serikali kulinda na kuhifadhi maliasili za nchi kwa kutoingiza mifugo, kufanya shughuli za binadamu hatarishi hususan wakati wa kuandaa mashamba kwa ajili ya kilimo.
“Kuingiza mifugo mwiko kwenye maeneo ya mifugo sababu atakayenufaika ni mfugaji kwa wakati ule, wanaingiza mifugo maelfu kwa maelfu upande wa Usangu na Ihefu. Lazima tulinde sababu mabonde hayo yanapeleka maji katika Bwawa la Kufua Umeme la Mwalimu Julius Nyerere,” amesema Balozi Pindi.
Leave a comment