SERIKALI inatarajia kutangaza rasilimali na bidhaa zinazozalishwa nchini, katika maonesho ya sita ya kimataifa ya biashara yanayofanyika jijini Dubai katika Nchi ya Umoja wa Falme za Kiarabu (UAE). Anaripoti Regina Mkonde, Dar es Salaam … (endelea).
Hayo yamesemwa leo Jumatano, tarehe 6 Oktoba 2021, Dar es Salaam, katika semina iliyoandaliwa na Mamlaka ya Maendeleo ya Biashara Tanzania (TanTrade), kuwajengea uwezo wahariri wa vyombo vya habari Tanzania kuhusu maonesho hayo.
Akizungumza katika semina hiyo, Msemaji Mkuu wa Serikali, Gerson Msigwa amesema kupitia maonesho hayo Tanzania itatangaza miradi ya kimkakati inayoitekeleza kwa ajili ya kuboresha mazingira ya uwekezaji, ikiwemo ya uzalishaji nishati ya umeme na miundombinu ya barabara.
Msigwa amesema katika maonesho hayo, Tanzania itatangaza mradi wa ujenzi wa Bwawa la Kufua Umeme la Julius Nyerere, reli ya kisasa (Standard Gauge).
“Hapa nchini moja ya vitu vinavyotuangusha ni umeme, wawekezaji wengi wakijua nchi haina nishati ya kutosha wanabadilisha msimamo. Hivyo katika maonesho hayo tutatangaza miradi ya kimkakati inayotekelezwa na Serikali,” amesema Msigwa.
Msigwa ameviomba vyombo vya habari kushirikiana na Tantrade kutangaza shughuli mbalimbali zinazofanywa na Tanzania katika maonesho hayo.
Naye Mkurugenzi Mkuu wa Tantrade, Latifah … amesema watayatumia maonesho hayo kutangaza rasilimali, vivutio vya utalii na bidhaa zinazopatikana Tanzania.
“Kipindi hiki cha maonehso ni malaum kwa ajili ya kui-brand Tanzania na ku-brand bidhaa za Watanzania. Muoneshe nguvu katika maonesho hayo kama mnavyofahamu lengo la Rais Samia Suluhu Hassan ni kui-brand Tanzania kimataifa, kupitia haya maonesho tunatangaza viwanda vyetu na bidhaa za Tanzania na tuna uwezo wa kuzalisha bidhaa gani,” amesema Latifa.
Amesema, Serikali ya Tanzania imetumia zaidi ya Sh. 700 milioni, kushiriki maonesho hayo.
Tanzania ni miongoni mwa nchi 191 zilizojisajili kushiriki maonesho hayo ya kimataifa, yanayofanyika kuanzia Oktoba 2021 hadi Machi 2022, ambapo imepangiwa kujinadi tarehe 26 Februari 2022.
Aidha, Kaimu Mkurugenzi Ukuzaji Biashara TanTrade, Getrude Ng’weshemi akitoa mada kuhusu maonesho hayo, amesema zaidi ya kampuni 600 zitapata nafasi ya kutangaza bidhaa zao kwa wageni 207,600 wanaotarajiwa kutembelea banda la Tanzania.
Ng’wesehemi amesema Tanzania imechagua katika eneo la uunganishaji, katika masuala ya uzalishaji masoko, uimarishwaji mawasiliano kati ya watu, bidhaa na teknolojia pamoja na kuchochea ujenzi wa miundombinu na kuchochea ukuaji wa biashara na utalii.
Amesema lengo la kushiriki maonesho hayo ni, kutangaza fursa za uwekezaji, masoko na bidhaa, utalii, maliasili, utamaduni, mila na desturi zinazopatikana nchini.
Pamoja na kujifunza mambo mbalimbali ya kibiashara na teknolojia.
Akielezea manufaa ya maonesho hayo kwa Tanzania, amesema itasaidia nchi kupata wawekezaji wapya na wadau wa biashara pamoja na watalii.
Amesema maonesho hayo yataimarisha mahusiano ya kidiplomasia kati ya Tanzania na mataifa yanayoshiriki maonesho hayo.
Pia, Tanzania itatangaza miradi ya maendeleo ya kimkakati inayotekelezwa na Serikali, ikiwemo bwawa la Nyerere.
Leave a comment