SERIKALI ya Tanzania, inatarajia kuanzisha mradi wa kuiuzia gesi Kenya. Anaripoti Regina Mkonde, Dar es Salaam…(endelea).
Hayo yamesemwa leo Ijumaa, tarehe 10 Desemba 2021 na marais wa mataifa hayo, Samia Suluhu Hassan wa Tanzania na Uhuru Kenyatta wa Kenya.
Ni baada ya mazungumzo yao ya faragha baina ya Samia na Kenyatta na baadaye kushirikisha viongozi wa pande zote mbili, yaliyofanyikia Ikulu jijini Dar es Salaam, Tanzania.
Mbele ya waandishi wa habari, Rais Samia amesema, mawaziri wa nishati wa nchi zote mbili, wameagizwa kusimamia ujenzi wa mradi huo, ambapo litajengwa bomba litakalosafirisha gesi kutoka Tanzania kwenda Mombasa Kenya.
“Kwa hiyo tutalaza bomba kutoka Tanzania kwenda Mombasa kusafirisha gesi, ili ikazalishe steamer lakini pia na gesi za kupikia majumbani, huo mradi tumewaachia mawaziri wamalize halafu ngazi za juu tutakuja kumalizia ili huo mradi uweze kuanza,” amesema Rais Samia.
Rais Samia amesema, Tanzania imeamua kupeleka gesi yake Kenya, ili kuwasaidia wananchi wake kuachana na matumizi ya mafuta, yanayoharibu mazingira.
“Kuna mradi wa gesi kutoka Tanzania kwenda Kenya na tumewaachia mawaziri wa nishati walishughulikie kwa sababu wenzetu wa Mombasa wanapta steamer (mvuke) yao kwa kutumia mafuta. Ulimwengu unatupigia kelele kuachana na nishati inayotokana mafuta wenzetu Kenya, Mungu hawakubaliki kupata gesi sisi tunayo,” amesema Rais Samia.
Kwa upande wake, Rais Kenyatta, amesema mradi huo utanufaisha wananchi wa Kenya na Tanzaia.
“Tumezungumza kwa njia gani tutaweza kununua gesi ambayo Mungu ameipatia nchi ya Tanzania na sisi badala ya kutumia mafuta kutoka nchi za nje, kupatia wananchi wetu steamer na kwa njia ambayo haisababishi mabadiliko ya tabia ya nchi,” amesema Rais Kenyatta na kuongeza:
“Hakuna haja ya sisi kununua haya mafuta, yastahili tununue gesi ya Tanzania. Hiyo ni faida kwa Tanzania, lakini pia faidi kwa Wakenya sababu watakuwa na clean energy sorce (chanzo kisafi cha nishati) na cheaper enegy sorce (chanzo nafuu cha nishati), ambayo itasaidia kuinua hali yao ya maisha.”
Leave a comment