MAKAMU wa Pili wa Rais wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar, Hemed Suleiman Abdulla, amesema Tanzania itafanya sensa ya aina yake na kuwa mfano kwa nchi zingine kuja kujifunza. Anaripoti Mwandishi Wetu, Iringa … (endelea).
Abdulla ambaye ni Mwenyekiti Mwenza wa Kamati ya Kitaifa ya Sensa ya mwaka 2022, ameyasema hayo leo Alhamisi tarehe Mosi, Julai, 2022 akifunga mafunzo ya Kitaifa ya sensa.
Amesema Tanzania ina historia kubwa na mwendelezo wa kufanya sensa ya watu na makazi tangu 1910.
Hata hivyo amesema sensa ya kisayansi ilianza baada ya muungano wa Tanganyika na Zanzibar ambapo ya kwanza ilifanyika mwaka 1967 na baadae mwaka 1976, 1988, 2002, na 2012.
“Hivyo sasa 2022 ni sensa ya sita kufanyika tangu mwaka 1964 hii ni wazi kwamba tuna uzoefu wa kutosha hapa nchini kwetu katika zoezi hili.
“Na ndiyo maana tumesema mwaka huu Tanzania tutafanya sensa ambayo nchi nyingine watakuja kujifunza Tanzania,” amesema.
Amesema sensa ya watu na makazi ya mwaka 2022 ni ya aina yake kwani itafanyika kidijitali na itakayounganisha mazoezi mawili makubwa ambayo hayajawahi kufanyika nchini tangu Muungano wa Tanganyika na Zanzibar 1964.
“Hii ni kwasababu sensa hii imeunganisha sensa ya majengo yote nchini na sensa ya anwani ya makazi.”
Abdulla amesema hadi sasa maandalizi ya sensa ya watu na makazi yamefikia asilimia 87 kuelekea tarehe 23 Agosti 2022.
“Hii ni hatua nzuri ambayo wananchi hatuna budu kuunga mkono serikali yetu na kuhakikisha zoezi hili linafanikiwa kwa kutoa ushirikiano kwa wasimamizi na makarani wetu wa sensa watakapozitembelea kaya zetu,” amesema.
Amesema kwa mujibu wa kanuni za Umoja wa Mataifa za kufanya tafiti za sensa za watu na makazi ni lazima watu wenye wa fani mbalimbali wakiwemo serikalini na sekta binafsi, asasi zisizo za kiraia, na vyuo vikuu watakaosimamia sensa kushiriki mafunzo.
Amefafanua lengo ni kujenga welewa mpana na wa pamoja wa wahusika hao kuhusu namna ya kukusanya takwimu nchi nzima kwa kutumia kanuni ya umoja wa mataifa zilizoainishwa.
“Bila kufanya hivyo matokeo yatakayotokana na sensa hayakubaliki kutumika ndani na nje ya nchi katika utekelezaji wa malengo ya dunia ya mwaka 2030 na ajenda ya Afrika ya mwaka 2063,” amesema.
Leave a comment