JESHI la Polisi, Kanda Maalumu ya Dar es Salaam limesema, litashirikiana na Shirika la Polisi la Kimataifa (INTERPOL) kuchunguza tukio la kupotea na kupatikana kwa raia wa Kenya, Raphael Ongangi. Anaripoti Regina Mkonde … (endelea).
Kauli hiyo imetolewa na Lazaro Mambosasa, Kamanda wa Polisi wa Kanda Maalumu ya Dar es Salaam wakati kizungumza na wanahabari leo tarehe 4 Julai 2019 jijini Dar es Salaam.
Kamanda Mambosasa amesema, Mkuu wa Jeshi la Polisi nchini, IGP Simon Sirro amempa maelekezo ya kufanya kuhusu tukio hilo kwa kuwa, taarifa zake zina utata, kutokana na mazingira aliyopatikana Ongangi ambaye alikuwa Msaidizi wa Zitto Kabwe, Kiongozi Mkuu wa Chama cha ACT-Wazalendo.
Kamanda Mambosasa ameeleza mashaka hayo, ikiwemo Ongangi kupatikana karibu na nyumba ya shangazi yake, mjini Mombasa nchini Kenya.
“Tunaendelea kufuatilia, taarifa zenyewe zimetolewa kwa mashaka makubwa. Tunaendelea kuunganisha na watu wa Interpol, kupitia Interpol tutawafikia Kenya ili kuangalia mazingira ambayo mhusika amepatikana tena karibu na nyumba ya shangazi yake,” amesema Kamanda Mambosasa.
Aidha, Kamanda Mambosasa amesema, mwaka juzi mtoa taarifa ambaye hakumtaja jina, aliwahi kutoa taarifa za kutaka kutekwa, lakini Jeshi la Polisi lilipofuatilia, lilibaini kwamba taarifa hizo zilikuwa za uongo.
“Mtoa taarifa mwaka juzi wakati nikiwa Dodoma, aliwahi sema kwamba yeye mwenyewe anataka kutekwa, lakini nilimwambia jeshi linafuatilia… na ukitaka kujiteka labda ujiteke mwenyewe,”amesema Kamanda Mambosasa.
Ameeleza kuwa, kutokana ma taarifa hizo kuwa na utata, uchunguzi ukibainisha kwamba tukio lilikuwa la kutengenezwa, wahusikawatachukuliwa hatua za kisheria.
Ongangi alitekwa tarehe 24 Juni 2019, jijini Dar es Salaam na kupatikana tarehe 1 Julai 2019 mjini Mombasa, Kenya.
Leave a comment