SERIKALI ya Tanzania imesema, jitihada zinaendelea kufanyika ili kumaliza tatizo la wakimbizi nchini humo kwa kuwarejesha makwao kwa kushirikiana na Jumuiya za Kimataifa na nchi wanazotoka. Anaripoti Jemima Samwel, DMC…(endelea).
Mara baada ya wakimbizi hao kuondoka, maeneo yote ya kambi za wakimbizi yatarejeshwa serikalini ili mamlaka zinazohusika ziweze kuyapangia matumizi stahiki.
Hayo yamesemwa leo Jumanne, tarehe 27 Aprili 2021, bungeni jijini Dodoma na Naibu Waziri wa Mambo ya Ndani, Khamis Chilo wakatio akijibu swali la Agustine Holle, Mbunge wa Kasulu Vijijini (CCM).
“Kumekuwa na mgogoro wa ardhi wa muda mrefu baina ya kambi ya wakimbizi ya Nyarugusu na Kata ya Makere, je ni lini Serikali itatatua mgogoro huo,” ameuliza Holle
Akijibu swali hilo, naibu waziri wa wizara hiyo, Chilo amesema, kambi ya wakimbizi ya Nyarugusu ilianzishwa mwaka 1996, kwa ajili ya kupokea wakimbizi kutoka nchi ya DRC.
Amesema, wakati wa uanzishwaji wa kambi hiyo, hakukuwa na mgogoro wa ardhi kwa sababu, lilikuwa eneo lisilotumika aidha pamoja na eneo la kambi, Serikali lilitenga eneo lingine la akiba kwa ajili ya wakimbizi iwapo eneo la awali litazidiwa.
“Kadri muda unavyokwenda, wananchi walianza kuvamia eneo la akiba kwa lengo la kuwatumia wakimbizi kama vibarua katika shughuli za kilimo katika eneo hilo.”
“Kwa kuzingatia maelezo hayo, ni wazi hakuna mgogoro wa ardhi baina ya kambi ya Nyarugusu na kata ya Makere, bali ni suala la uelewa ambapo wananchi wanaendelea kuelimishwa juu ya matumizi ya eneo hilo,” amesema Chilo
Leave a comment