SERIKALI imesema hadi kufikia mwaka 2022 Tanzania ilikuwa na jumla ya maprofesa 226 kati yao 163 wakiwa ni maprofesa washiriki (Associate Professors) na 63 ni maprofesa kamili (Full Professors). Anaripoti Mlelwa Kiwale, TUDARCo…(endelea).
Hayo yameelezwa leo Jumanne bungeni jijini Dodoma na Naibu Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, Juma Kipanga.
Kipanga alikuwa anajibu swali Mbunge wa Muleba Kusini, Oscar Kikoyo (CCM) aliyetaka kufahamu ni maprofesa wangapi wanaozalishwa nchini kila mwaka na ni wangapi wanastaafu kwa kipindi hicho.
Naibu Waziri huyo, amesema profesa ni ngazi ya juu ya kitaaluma ambapo mhadhiri au mtumishi wa taasisi za elimu ya juu hufikia baada ya matokeo ya kazi ya kitaaluma ikiwemo kufanya machapisho ya ufundishaji.
Hivyo, kupanda cheo kwa mwanataaluma kunatokana na jitihada za mhusika katika ufundishaji, kufanya tafiti na kuchapisha maandiko yake kwenye majarida yanayokubalika kitaifa na kimataifa.
“Hivyo kuongezeka kwa idadi yao kunategemea zaidi jitihada za mtu binafsi katika utekelezaji wa majukumu yake na kukubalika kwa jitihada hizo kwa wanataaluma wenziwe kwa kuzingatia miongozo waliyojiwekea.
Kipanga ameongeza kuwa suala la kustaafu linahusu zaidi vyuo vikuu vya umma ambao umri wa kustaafu ni miaka 65, kwa takwimu za mwaka 2022.
Amesema idadi ya maprofesa kamili waliostaafu ni wanne na wanaotarajiwa kustaafu kwa mwaka 2023 ni watano, mwaka 2024 ni wawili na mwaka 2025 ni sita.
“Maprofesa washiriki waliostaafu kwa mwaka 2022 ni mmoja na wanaotarajiwa kustaafu kwa mwaka 2023 ni 18, mwaka 2024 ni wanne na mwaka 2025 ni sita,” amesema.
Katika maswali ya nyongeza, Kikoyo aliitaka serikali ibadili umri wa kustaafu kutoka miaka 65 mpaka miaka 70 ili kutunza hao wachache waliopo kutokana uhitaji mkubwa wa maprofesa.
“Kwanini isitoe package nzuri ili kuwavutia vijana wengi wakajitahidi, wakafanya research ili waweze kufikia hiyo hatua ya uprofesa kwa ajili ya kutunza vyuo vyetu vikuu? Alihoji Kikoyo.
Akijibu maswali hayo, Kipanga amesema umri wa wanataaluma kustaafu hususani maprofesa uliongezwa kutoka miaka 60 mpaka 65 hivyo suala la kufikia miaka 70 wanachukua ushauri huo na kwenda kuufanyia kazi ili kuangalia namna bora ya kufanya.
Leave a comment