BODI ya kahawa Tanzania inakusudia kuongeza uzalishaji kutoka tani 80,000 za mwaka 2017 hadi kufikia tani 100,000 mwaka 2021, anaandika Christina Haule.
Hayo yamebainishwa leo na Primus Kimario, Kaimu Mkurugenzi mkuu wa Bodi ya Kahawa Tanzania wakati akizungumza kwenye mkutano mkuu wa nane wa wadau wa kahawa uliofanyika mkoani Morogoro.
“Uzalishaji wa zao hilo mwaka 2016 ulishuka na kuzalisha tani 46,000 tofauti na mwaka 2015 ambapo Bodi ilizalishwa tani 60,000 jambo lililoilazimu bodi hiyo kusimamia utafiti wa zao hilo na kuona namna ya kuongeza uzalishaji ili kuleta tija kwa mkulima na kukuza uchumi wa Taifa,”amesema.
Katika kuboresha uzalishaji huo Kimario amesema waliwaomba wakulima kuona umuhimu wa kutumia miche ya kahawa ya kisasa yenye uwezo wa kuongeza uzalishaji na kuongeza pato kwa 15% kwa mkulima tofauti na miche ya kizamani ya Arabika.
Dk. Deusdedit Kilambo, Mtafiti kutoka sekta ya maendeleo ya utafiti wa kahawa nchini TaCRI amesema, tayari wameshafanya utafiti wa miche sahihi ya kahawa na kupata aina 23 bora za kahawa duniani.
Aidha, Amefafanua kuwa kati ya aina hizo mpya 19 za Arabika na 4 za Robusta wameweza kutafiti, kuzalisha na kusambaza miche aina ya Chotara (ya kupandikiza kwenye chupa) zoezi ambalo limeenda sambamba na utafiti wa udongo nchi nzima ambapo wamepata wilaya 42 kati ya mikoa 14 zenye uwezo wa kulimwa zao hilo.
Leave a comment