WAKATI uchaguzi wa serikali za mitaa 2019, ukitarajiwa kufanyika Novemba mwaka huu, Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (Tamisemi) imewataka wadau wa vyama vya siasa, kutoa maoni yenye tija kwa ajili ya rasimu za kanuni za uchaguzi huo. Anaripoti Danson Kaijage, Dodoma … (endelea).
Rai hiyo imetolewa leo tarehe 1 Aprili 2019 na Selemani Jafo, Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Tamisemi katika kikao kazi cha kupitia rasimu za kanuni za uchaguzi wa serikali za mitaa mwaka 2019, jijini Dodoma.
Kikao hicho cha siku mbili kimekutanisha wadau wa vyama vya siasa, ikiwemo Baraza la Vyama vya Siasa, Msajili wa Vyama hivyo, Tume ya Uchaguzi na wizara mbalimbali.
Akifungua kikao hicho, Jafo alitaja rasimu tatu ambazo wadau hao watazijadili kuwa ni pamoja na Rasimu ya Kanuni za Uchaguzi wa Mwenyekiti wa Kijiji, Wajumbe wa Halmashauri ya Kijiji na Mwenyekiti wa Kitongoji katika Mamlaka za Wilaya za mwaka 2019.
Ametaja rasimu zingine kuwa ni ya Uchaguzi wa Mwenyekiti wa Mtaa na Wajumbe wa Kamati ya Mtaa katika Mamlaka za Miji za mwaka 2019 na Rasimu ya Kanuni za Uchaguzi wa Mwenyekiti wa Kitongoji katika Mamlaka za Miji Midogo za mwaka 2019.
“Tunaimani nyie wadau wa vyama vya siasa mtatoa maoni yenye tija ili kutengeneza kanuni zilizo bora zitakazosimamia uchaguzi wa serikali za mitaa, uchaguzi huu unatarajia kufanyika muda wote kati ya Novemba huu,”amesema.
Amesema, Tanzania inaongozwa kwa utaratibu wa demokrasia, hivyo serikali iliona ni vyema kutengeneza jukwaa la kuwakutanisha wadau mbalimbali, wakiwemo vyama vya saisa ili kuwa na kanuni bora zitakazoendesha uchaguzi kwa amani na utulivu.
“Niliona sio vyema kwa mujibu wa utaratibu wa uundwaji wa kanuni hizi, lazima tuunde kanuni ambazo zinamchango mkubwa wa wadau mbalimbali ambao utasaidia sana katika mwenendo wa uchaguzi tunaoendana nao,”alisema.
John Shibuda, Mwenyekiti wa Baraza la Vyama vya Siasa amesema, watahakikisha wanatengeneza kanuni zitakazojenga taswira nzuri ya nchi Kitaifa na Kimataifa.
Ameomba katika kikao hicho, msajili wa vyama atoe uwianishaji wa kanuni hizo pamoja na sheria mpya ya vyama vya siasa ili isisababishe msuguano wakati wa uchaguzi huo.
“Ili kuondokana na dukuduku na sintofahamu kuwepo uwianishaji wa sheria ya vyama vya siasa na kanuni hizi za uchaguzi, tuongeze muda wa majadiliano uwe siku tatu ili tumsikie msajili anasemaje kwenye hili ili isitokee misuguano,” amesema.
Leave a comment