NAIBU Waziri wa Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (Tamisemi) nchini Tanzania, Mwita Waitara amemuagiza Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Paul Makonda, kufanya uchunguzi wa upotevu wa Sh.1.6 bilioni, zilizoibuliwa na Boniface Jacob, aliyekuwa Meya wa Halmashauri ya Ubungo. Anaripoti Mwandishi Wetu …(endeelea).
Wiki iliyopita, Jacob akizungumza na waandishi wa habari jijini Dar es Salaam alisema, miongoni mwa sababu zilizotumika kumwondoa madarakani ni jitihada zake za kuibua ufisadi bilioni hizo za fedha.
Jacob amepoteza nafasi ya umeya baada ya barua inayoelezwa kuandikwa tarehe 28 Aprili 2020 na katibu wa Chadema Kata ya Ubungo kwenda kwa mkurugenzi wa halmashauri kuonyesha amevuliwa uanachama hivyo kupoteza sifa za kuwa meya.
Hata hivyo, Jacob mwenyewe, Chadema makao makuu na mtu huyo ambaye jina lake lilitumika kwenye barua hiyo kudai haina ukweli kwani hakuna kikao chochote kilichokaa cha kumjadili Jacob kisha kumvua uanachama.
Akizungumza na MwanaHALISI Online leo Jumatatu tarehe 11 Mei 2020, Waitara amesema kama kumetokea wizi au upotevu wowote wa fedha kwenye Halmashauri hiyo ni lazima Meya ahusike kwa kuwa yeye ni sehemu ya watia saini.
Amesema hakuna malalamiko yoyote yaliyofikishwa ofisi ya mkuu wa mkoa au katibu tawala wa mkoa kuhusu upotevu wa fedha hizo.
Waitara amesema kwa kuwa Jacob ametoa tuhuma hizo hadharani, atakuwa na vithibitisho hivyo ameagiza uchunguzi ufanyike na watakaobainika hatua zitachukuliwa dhidi ya wale wote waliohusika ikiwamo Jacob mwenyewe.
“Serikali inafanya uchunguzi zaidi na kwamba itamchukulia hatua kwa upotoshajikwa sababu yeye kipindi chote tangu mwaka 2016 alipokuwa Meya asisema kama kuna upotevu mpaka pale chama chake kilipomvua uanachama ndio aseme,” amesema Waitara
“Jacob ni kama mfamaji tu, haishi kutapata…yeye ni sehemu ya watia saini wa miradi yote ndani ya Halmashauri, hivyo ni lazima itakuwa kahusika kwenye upotevu huo,” amesema Waitara.
Baada ya Jacob kung’olewa katika nafasi hiyo, Tamisemi ilimweleza ana njia mbili za kuchukua ambazo ni kufungua kesi mahakamani au kukata rufaa kwa waziri wa Tamisemi.
Waitara akijibu swali la MwanaHALISI Online lililotaka kujua kama barua imekwisha kufika amesema hadi leo Jumatatu asubuhi ilikuwa haijafika.
Leave a comment