MKURUGENZI wa Ofisi ya Taifa ya Takwimu (NBS), Daktari Albina Chuwa, amesema takwimu za sensa ya watu na makazi za 2022, zitasaidia kuondoa masharti magumu ya mikopo inayotolewa na taasisi za kifedha nchini, kwa kuwa zina taarifa muhimu za waombaji. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dodoma … (endelea).
Dk. Chuwa amesema hayo leo Jumatatu, tarehe 31 Oktoba 2022, jijini Dodoma katika uzinduzi wa matokeo ya sensa ya watu na makazi, iliyofanyika tarehe 23 Agosti mwaka huu. Uzinduzi huo umefanywa na Rais Samia Suluhu Hassan.
Mkurugenzi huyo wa Takwimu amesema, kupitia zoezi la anuani za makazi, NBS ilikusanya takwimu za wafanyabiashara na wajasiriamali na kuanzisha kanzi data inayoonyesha biashara zao na mahali zilipo.
“Matokeo haya yanafikia sekta mbalimbali ya kiuchumi na kimazingira, gavana wa benki kuu yupo hapa katika kampeni yetu ya kuinua kina mama, vijana na wazee kwenye mikopo hatutahitaji tena masharti magumu ya mikopo kupitia hati za viwanja,”
“Kupitia operesheni ya anuani za makazi, tumechukua takwimu tunayo kanzi data inayoonesha biashara ziko sehemu gani hivyo ni rahisi sekta ya kibenki kutoa mikopo ya kutosha,” amesema Dk. Chuwa.
Aidha, Dk. Chuwa ameshauri muongozo wa kitaifa wa matumizi ya sensa utumike ipasavyo kuanzia ngazi ya kitaifa hadi vitongoji, kwa ajili ya kuwaletea maendeleo wananchi.
Leave a comment