TAASISI ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (Takukuru) nchini Tanzania yatoa onyo kwa watu wanaowarubuni waliojiandikisha kupiga kura kwenye Uchaguzi Mkuu utakaofanyika Jumatano 28 Oktoba 2020 kuacha mara moja. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dar es Salaam…(endelea)
Takukuru imesema, atakayebainika atakamatwa na atachukuliwa hatua kali za kisheria ikiwa ni pamoja na kufikishwa mahakamani.
Hayo yamesemwa leo Jumatano tarehe 30 Septemba 2020 na Doreen Kapwani, Afisa Uhusiano wa Takukuru kwa niaba ya Mkurugenzi Mkuu wa Taasisi hiyo, Brigedia Jenerali, John Mbungo.
Doreen amesema, zipo taarifa baadhi ya wapiga kura wamekuwa wakirubuniwa na wajanja wachache wenye nia ovu ya kuwaondolea wananchi hao haki yao ya msingi na ya Kikatiba ya kupiga kura.
Amesema, inadaiwa wananchi wanaorubuniwa ni wale waliojiandikisha kwenye daftari la kupiga kura na kuwa na sifa zote za kuwawezesha kupiga kura lakini kwa kurubuniwa na baadhi ya wajanja, wananchi hao wanakubali kuzitoa kadi zao kwa ahadi mbalimbali.
Doreen amezitaja ahadi hizo ni; wapo wanaoahidiwa kupatiwa mikopo baada ya kuzikabidhi kadi hizo, wapo wanaoahidiwa kupewa fedha tasilimu na wapo wanaoahidiwa kutunziwa kadi hizo hadi tarehe 28 Oktoba 2020 ambayo ni siku ya kupiga kura.
“Tunawaasa wanaojihusisha na vitendo hivyo kuacha mara moja kwani atakayebainika atakamatwa na atachukuliwa hatua kali za kisheria ikiwa ni pamoja na kufikishwa mahakamani,” amesema Doreen
Leave a comment