MWANACHAMA wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), anayejipanga kugombea ubunge katika Jimbo la Ubungo, jijini Dar es Salaam (jina tunalo), amewatoroka Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (Takukuru). Anaripoti Mwandishi Wetu, Dar es Salaam … (endelea).
Katika tukio hilo lililotokea jana jioni tarehe 31 Mei 2020, viongozi wanne wa chama hicho katika jimbo hilo, wanashikiliwa na Takukuru wilaya ya Ubungo.
Taarifa ambazo MwanaHALISI Online ilizopata leo Jumatatu tarehe 1 Juni, 2020 zinaeleza, viongozi hao wanatuhumiwa; kutoa rushwa na kuanza kampeni za uchaguzi mkuu Oktoba 2020 kabla ya wakati.
Msiri wa mtandao huu ameeleza, wakati wa mtego huo, mmoja kati yao alikurupuka na kukimbia na kutelekeza gari, kwenye tukio hilo viongozi wanne wamekamatwa.
“Walikuwa na mtu mmoja mmama anayetaka kugombea ubunge Ubungo, lakini yeye alikimbia ila akaacha gari na wenzake wanne ambao ni viongozi mbalimbali jimboni humo wakakamatwa na Takukuru wa Ubungo,” ameeleza.
MwanaHALISI Online limemtafuta Emmanuel Tarmo Boay, Kamanda wa Takukuru Wilaya ya Ubungo ili kupata ufafanuzi wake, amesema “suala hilo siwezi kulizungumzia mimi, atafutwe Kamanda wa Takukuru Mkoa wa Kinondoni ambaye ndiye mzungumzaje wa mkoa.”
Pili Mwakasege, Kamanda wa Takukuru Mkoa wa Kinondoni alipotafutwa, amesema suala hilo atalitolea ufafanuzi, “tutatoa taarifa rasmi. Tuko kazini.”
Endelea kufuatilia MwanaHALISI ONELINE kwa habari zaidi
Leave a comment