WAKULIMA 2,176 katika Mkoa Morogoro, Iringa na Jombe, wamenufaika na mafunzo stadi katika kilimo na ufugaji, yaliyotolewa kupitia mradi wa Tajirika na Kilimo unaotekelezwa na Mamlaka ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi Stadi (VETA), ikishirikiana na Shirika la Kimataifa la CARE na Taasisi ya Ukuzaji Kilimo Uwanda wa Kusini mwa Tanzania (SAGCOT). Anaripoti Mwandishi Wetu, Dodoma … (endelea).
Akizungumza wakati wa kikao cha tathmini ya utekelezaji wa mradi huo jijini Dodoma, Mratibu kutoka VETA, Perecy Ugula, alisema wakulima hao walipatiwa mafunzo ya ufugaji bora wa mifugo, hasa ng’ombe wa maziwa na kuku, kilimo cha mazao mchanganyiko, kilimo cha mbogamboga na matunda.
Ugula alisema, mafunzo hayo yamefanikiwa kubadili uendeshaji wa shughuli za wakulima hao kuwa za kisasa na za kibiashara.”Wakulima 2,176, wanawake (1,294) na wanaume (882) wa mikoa ya Morogoro, Iringa na Njombe, wamepata mafunzo ya ufugaji na kilimo bora kupitia Mradi wa Tajirika na Kilimo,” alisema Ugula.
Ugula alitaja mafanikio mengine yaliyopatikana kwenye mradi huo, ni pamoja na uandaaji wa mitaala miwili ya sekta ya kilimo, ambayo ni Mtaala wa Kilimo cha Mbogamboga na Matunda.
Na Mtaala wa Kilimo cha Mazao na kuuboresha mtaala wa Afya na Ufugaji wa Mifugo.
Kwa upande wake, Afisa Tathmini na Ufuatiliaji wa Shirika la Kimataifa la CARE, Edwin Sallu, alisema kupitia utekelezaji wa mradi huo wamegundua uwepo wa uhitaji mkubwa wa mafunzo ya stadi za kuboresha shughuli za kilimo, kwa wakulima wadogo wa vijijini.
Na kwamba wengi wao wako tayari kugharamia mafunzo hayo, kama inavyofanyika sasa katika Mradi wa Tajirika na Kilimo.
Ofisa huyo, ameiomba VETA kupanua zaidi wigo wa mafunzo kwa mfumo wa kuwafuata wahusika, katika maeneo yao vijijini.
Sallu alisema, mafunzo hayo yamewezesha kuunda vikundi 141 vya uzalishaji katika sekta ya kilimo cha mazao mchanganyiko, mbogamboga, matunda na ufugaji wa kibiashara, ambavyo kwa sasa vinafanya shughuli zake za kilimo kwa pamoja.
Pia, Sallu alisema uzalishaji mazao kwa sasa umeongezeka, huku yakiwa na ubora sambamba na uhakika wa kufikia masoko ya bidhaa zao na kuwezesha wakulima hao kukopesheka kwa urahisi na kupata faida nzuri.
“Kwa kweli tumeshuhudia manufaa makubwa ya mafunzo yaliyotolewa kupitia mradi huu kwa wakulima vijijini, hasa ukizingatia kuwa asilimia 67 ya wanufaika ni wanawake na watoto wa kike ambao tunaamini wataleta mabadiliko chanya kwenye jamii zao,” alisema Sallu.
Meneja wa Kongani ya Kilombero kutoka Taasisi ya SAGCOT, John Nakei, alisema taasisi yake itaendelea kutoa ushauri, kuwaunganisha na fursa za masoko na kutoa elimu zaidi kwa wakulima katika mikoa hiyo, ili kuwasaidia kuendesha shughuli za kilimo kwa tija zaidi na kuwezesha uzalishaji endelevu wa chakula.
Kwa upande wake, Mkurugenzi Msaidizi wa Huduma za Ugani kutoka Wizara ya Mifugo na Uvuvi, Dk. Kejeri Gillah, licha ya kuwapongeza wadau katika utekelezaji wa mradi huo, ameshauri kuweka mkakati wa uendelezaji wa shughuli zilizofanywa kwenye mradi huo, ili wakulima wengi zaidi wanufaike na mafunzo hayo.
Mkurugenzi wa VETA Kanda ya Nyanda za Juu, Susan Magani, alisema VETA inaendelea na jitihada mbalimbali za kuhakikisha mafunzo ya ufundi stadi yanawafikia wananchi wengi zaidi, hasa maeneo ya vijijini.
Na kwamba anaamini kuwa wakulima wengi zaidi nchini, watanufaika na mafunzo hayo ili kuboresha shughuli zao.
Mradi wa Tajirika na Kilimo ulianza kutekelezwa mwaka 2018 kwa lengo la kujenga na kuimarisha ujuzi katika sekta ya kilimo kwa wakulima 2,200 na unatarajiwa kumalizika Desemba 2021.
Leave a comment