MUASISI wa kampuni ya magari ya Tesla, Elon Musk ambaye pia ni tajiri namba moja duniani, amenunua kampuni ya mtandao wa kijamii ya Twitter kwa dola za Kimarekani bilioni 44 (Sh trilioni 102.2). Anaripoti Rhoda Kanuti kwa msaada wa mitandao ya Kimataifa … (endelea).
Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa jana tarehe 25 Aprili, 2022 na mmoja wa wajumbe wa Bodi ya wakurugenzi wa kampuni hiyo, Bret Taylor imeeleza kuwa chini ya mkataba huo, wenye hisa watapokea dola 54.20 (Sh. 125,920) kwa kila hisa.
Makubaliano hayo yanatarajiwa kukamilika rasmi mwaka huu. Hii ina maana kuwa mojawapo ya makampuni makubwa kabisa ya mitandao ya kijamii duniani itamilikiwa na mtu mmoja.
Musk mwenye wafuasi zaidi ya milioni 84 katika mtandao huo, amesema atazingatia zaidi katika kuruhusu uhuru wa kujieleza kwenye jukwaa hilo.
Amesema alitaka kuumiliki mtandao huo wa kijamii na kuufanya kuwa wa kibinafsi kwa sababu anahisi kuwa hautimizi uwezo wake wa kuwa jukwaa la uhuru wa kujieleza.
Awali, kampuni hiyo inayomilikiwa na wanahisa mbalimbali, ilijaribu kulizuia pendekezo la Musk, lakini baada ya mkutano mrefu kati yake na wanahisa hao mwishoni mwa wiki iliyopita, ikaridhia ombi hilo.
Leave a comment