Moto umezuka katika mlima Kilimanjaro, karibu na eneo la Karanga Camp lililopo urefu wa meta 3,963 kutoka usawa wa bahari kupitia njia ya Mweka na jitihada ya kuuzima zinaendelea. Anaripoti Mwandishi Wetu, Kilimanjaro … (endelea).
Kwa mujibu wa Kamishina wa Uhifadhi kanda ya Kaskazini, Betrita James, chanzo cha moto huo bado hakijajulikana.
Amesema baada ya kupata taarifa za kuonekana kwa moto huo, menejimenti ya Kinapa ilianza mara kazi ya kukusanya nguvu kazi na vifaa, na tayari timu zimeelekea eneo hilo.
Mbali na timu hiyo, picha na video ambazo zimesambaa katika makundi mbalimbali ya Whatsapp zinawaonyesha baadhi ya waongoza watalii (Guides) na wapagazi (porters), wakijaribu kuzima moto huo kwa kutumia majani ya miti.
Hata hivyo, imeelezwa kuwa moto huo uko karibu na Karanga Camp na Askari wa Kinapa na wadau wengine walikuwa wakielekea huko kushiriki kazi ya kuuzima.
Oktoba 2020, moto mwingine ulizuka katika mlima huo katika ukanda wa nyasi na vichaka na kuteketeza vibanda 15 vya kulala wageni katika mlima Kilimanjaro pamoja na mifumo ya umeme wa jua na miundombinu ya maji taka.
Leave a comment