IMEELEZWA pamoja na Shirika la Posta kumilikiwa na serikali kwa asilimia 100, ni asilimia 20 tu ya taasisi za serikali ndio zinatumia huduma za shirika hilo, anaandika Nasra Abdallah.
Hayo yameelezwa Naibu Waziri Uchukuzi na Mawasiliano, Mhandisi Atashasta Nditiye, alipotombelea shirika hilo kujionea shughuli mbalimbali na changamoto zinazolikabili shirika hilo.
Mhandisi Nditiye amesema asilimia 20 ya taasisi za serikali kutumia shirika hilo hiyo ni ndogo ukilinganisha na idadi ya taasisi zilizopo na kuagiza kwamba kuanzia bsasa ni vema zikitumia huduma za shirika hilo.
Waziri huyo amesema endapo watatumia huduma hizo wataliwezesha shirika hilo kujiendesha na pia kuchangia pato la taifa kama yanavyofanya mashirika mengine yanayojiendesha kibiashara.
“Kuanzia sasa nataka kuona taasisi za serikali zinalitumia shirika hili ipasavyo kwani tofauti na huko nyuma hivi sasa limeboresha huduma zake na hawana sababu ya kutlitumia ili nalo liweze kujiendesha,” amesema Mhandisi Nditiye.
Kwa upande wake Kaimu Postamasta Mkuu, Hassan Mwang’ombe, ameelezea kuhusu changamoto zinalolikabili shirika hilo, kwa muda mrefu ni pamoja na kulipa madeni ambayo hawakustahili kuyalipia ikiwemo deni la wastaafu waliokuwa Jumuiya ya Afrika Mashariki.
Mwang’ombe amesema katika ulipaji huo wa viinua mgongo kila mwezi mpaka sasa hivi wameshalipa zaidi ya Sh. 3.9 bilioni ambazo kama wangezielekeza katika shughuli nyingine zingesaidia kuboresha huduma za shirika hilo ili kuendana na ushindani wa soko lililopo kwa sasa.
Naye Mwenyekiti wa bodi wa shirika hilo, Kanali Mstaafu, Haroun Kondo, ameahidi kuafanyia kazi maagizo yaliyotolewa na Waziri huyo ikiwemo kuongeza idadi ya wateja.
Kondo amesema katika harakati hizo tayari wameanza kuboresha huduma zao ikwemo kutenga fedha kiasi cha Sh. 1.2 bilioni kwa ajili ya kununulia mabasi katika awamu ya kwanza ya mwaka huu wa fedha ambayo amesema anaamini yatasaidia kuboresha huduma zao za utumaji vifurushi.
Leave a comment