WADAU wa taasisi za fedha mkoani Kilimanjaro, wameeleza kuwa changamoto ya mabadiliko ya kiuchumi imewasababishia wakose faida katika kipindi cha kuanzia mwaka jana, anaandika Mwandishi Wetu.
Mwenyekiti wa Bodi ya Benki ya Uchumi inayomilikiwa na Dayosisi ya Kaskazini ya Kanisa la Kiinjili la Kilutheri Tanzania (KKKT), Wilson Ndesanjo amesema hali hiyo imetokana na uamuzi wa serikali kurudisha fedha zake Benki Kuu (BOT).
Ndesanjo anasema “Idadi ya wananchi wanaoweka fedha zao katika taasisi za kifedha zikiwamo benki na vikundi vya ushirika vya kuweka na kukopa katika jamii imeshuka na hivyo kusababisha urejeshwaji wa mikopo kuwa mgumu,
Anaongeza,” Changamoto hiyo ya mabadiliko ya kiuchumi ndiyo imetufanya tukose faida katika kipindi cha kuanzia mwaka jana.”
Anasema mzunguko wa fedha kwa wafanyabiashara hivi sasa ni mgumu ikilinganishwa na miaka ya nyuma.
Kwa upande wake, Mkuu wa Kanisa la Kiinjli la Kilutheri Tanzania (KKKT), Askofu Dk. Fedrick Shoo akizungumzia hali hiyo alisema kuna haja ya viongozi wa taasisi za fedha kutumia teknolojia za kisasa katika kufanya biashara za kifedha ikiwa ni pamoja kuwafikia wananchi vijijini.
Meneja wa Benki hiyo ya Uchumi, Anjela Moshi alisema mpango wa utoaji huduma kwa njia ya simu za mikononi umekuwa mkombozi mkubwa kwa wananchi waishio maeneo ya vijijini hususani wakulima na wafugaji.
Leave a comment