TAASISI ya Kumbukumu ya Mwalimu Julius Nyerere, imeiomba Serikali, wadau na wananchi, watoe mchango wao wa hali na mali, kwa ajili ya ujenzi wa makumbusho ya mwasisi huyo wa Taifa la Tanzania, katika Jiji la Dar es Salaam. Anaripoti Regina Mkonde, Dar es Salaam … (endelea).
Wito huo umetolewa leo Alhamisi, tarehe 3 Machi 2022, jijini Dar es Salaam na Mwenyekiti wa Taasisi hiyo, Paul Kimiti, akitaja maandalizi kuelekea kumbukizi ya miaka 100 ya kuzaliwa Mwalimu Julius Nyerere, itakayofanyika tarehe 13 Aprili mwaka huu.
“Baba wa Taifa aliipigania Tanzania, sasa tusije fanya makosa, Dar es Salaam ni center (kituo) wote wanafika. Tulizungumza na wazee wa Butiama kwamba itabakia makumbusho,”
“Lakini ukitaka watu wafaidi wajue Mwalimu Nyerere alifanya nini lazima kuwe na jengo. Kama Watanzania tuchangie wote, kama wahisani watakuwepo watatusaidie lakini tufanye jambo ili falsafa ya Baba wa Taifa iendelee kudumu na watu waendelee kujifunza,” amesema Mzee Kimiti.
Kimiti amesema, Jiji la Dar es Salaam lina historia kubwa kwa Tanzania, kwa kuwa shughuli za uhuru wa Tanganyika zilifanyika.
“Dar es Salaam ndiyo center, wakati wa uhuru sherehe zote za uhuru zilifanyika Dar es Salaam, nataka niwaombeni, hakuna kitu muhimu kama kuifanya center kujenga makumbusho ya Baba wa Taifa. Wenzetu nchi nyingine kiongozi aliyewakomboa wanamjengea jengo pia inakuwa kitega uchumi, hela inapotolewa inasaidia walemavu, wasio na kazi na yatima,” amesema Kimiti.
Kimiti amesema kuelekea maadhimisho ya miaka 100 ya kuzaliwa Mwalimu Nyerere, wamepanga kuandaa makongamano katika kanda za Tanzania, ambapo kila eneo zitafanyika shughuli ambazo alikuwa anazifanya wakati wa uhai wake.
Amesema katika Kanda ya Ziwa, kongamano litafanyika mkoani Kagera, ambapo litazungumzia kuhusu vita ya Kagera. Watoa mada wataeleza mchango wa Mwalimu Nyerere, athari na faida za vita hiyo iliyopigwa kati ya Tanganyika na Uganda.
Kimiti amesema, kongamano lingine litafanyika wilayani Musoma Mkoa wa Mara, ambako sera ya elimu ilianzishwa.
“Tukitoka hapo tunaenda Kanda ya Kati, mkoani Dodoma. Baba wa Taifa alisema iwe makao makuu, tutaenda kueleza kwa nini aliamua iwe kule . Pia Wilaya ya Kongwa ilikuwa kituo cha wapigania uhuru, tunataka watu wajue maeneo hayo wasije wakasahau historia yao,” amesema Kimiti.
Kimiti amesema kongamano lingine litafanyika kwenye Kanda ya Kaskazini, ambako Azimio la Arusha lilianzishwa. Wadau watajadili mafanikio ya misingi ya azimio hilo, ambayo ilikuwa siasa ya ujamaa na kujitegemea.
Mwenyekiti huyo wa Taasisi ya Kumbukumbu ya Mwalimu Nyerere, amesema kongamano lingine litafanyika visiwani Zanzibar, ambako muungano wa Tanganyika na Zanzibar ulianzia. Kupitia kongamano hilo, changamoto na mafanikio ya muungano huo zitajadiliwa.
“Kanda nyingine ni ya Nyanda za Juu Kusini , Iringa ilikuwa center ya kuanzisha siasa na kilimo. Kanda hiyo itasaidia kujua siasa na kilimo imetusaidia nini, wapi tumekosea ili mafanikio yale baba alitaka yapatikane yanapatikanaje,” amesema Kimiti nakuongeza:
“Kusini ilikuwa center ya majeshi yetu ili wavamizi katika Kanda ya Kusini wasivamie. Kanda ya Magharibi tunasema ni muhimu sababu sera ya vijiji vya ujamaa imeanzia Rukwa na vijiji vya ujamaa vimeanza, vikasambaa nchi nzima.”
Naye Mjumbe wa Bodi ya Wakurugenzi ya taasisi hiyo, Balozi Francis Mndolwa, amesema taasisi hiyo ni msingi wa kuimarisha umoja wa Tanzania.
“Taasisi ilipoanzishwa nilikuwa mmoja wapo niliyojiunga sababu taasisi ni msingi wa kuimarisha umoja wetu. Taasisi hii imejitanua na ni ya kila mtu na nimejiunga kwa msingi kwamba taasisi inayounganisha watu wengi nami nikataka kuunganisha Watanzania ili kuimarisha uhuru wa nchi yetu,” amesema Balozi Mndolwa.
Leave a comment