MBUNGE wa Urambo, Magreth Sitta (CCM), ameihoji serikali ni kwanini haioni umuhimu wa kuunda taasisi ya kusimamia ubora wa elimu nchini, anaandika Dany Tibason.
Mbunge huyo alitoa hoja hiyo leo bungeni wakati alipokuwa akiuliza swali la nyongeza ili serikali iweze kulitolea ufafanuzi swali hilo.
Awali katika swali la msingi la mbunge huyo alitaka kujua ni kwanini serikali haiundi chombo kinachojitegemea cha ukaguzi wa elimu.
“Kwa mujibu wa takwimu za serikali kumekuwa na ongezeko kubwa la Taasisi za Elimu zikiwemo shule za serikali za msingi na sekondari, Shule Maalum, Vyuo vya Ualimu na vituo vya elimu ya watu wazima.
“Kwa kuzingatia kuwa ubora wa elimu ni suala la kipaumbele kwa watanzania wengi, Je kwanini serikali haiundi chombo kinachojitegemea cha ukaguzi wa elimu,” alihoji Sita.
Akijibu maswali hayo Naibu Waziri wa Elimu ya Sanasi na Teknolojia Mhandisi Stella Manyanya, amesema idara ya ukaguzi ya shule iliundwa kwa mujibu wa sheria ya elimu Sura ya 353 ya sheria ya nchi,ikiwa ni jukumu la kufuatilia ubora wa elimu ya msingi, sekondari na vyuo vya elimu kwa kuzingatia viwango vya utoaji wa elimu vilivyowekwa.
“Kwa kuwa idara ya ukaguzi wa shule ilianzishwa kwa mijibu wa sheria ya elimu kwa sasa Wizara inafanya mabadiliko ya sheria ya mfumo mzima wa elimu ili iende sambamba na sera ya Elimu ya mafunzo ya mwaka 2014,” alieleza Mhandisi Manyanya.
Amesema suala la ukaguzi wa shule kuwa chombo kinachojitegemea litaangaliwa kwa mapana katika hatua za kufanya mabadiliko ya sheria hiyo,pamoja na nyingine ambazo zitaweza kuongeza ufanisi katika ukaguzi wa shule.
Leave a comment