MGOMBEA Urais wa Chama cha Wanasheria wa Tanganyika (TLS), Harold Sungusia, amesema amejitosa katika kinyang’anyiro hicho, baada ya kuona chama hicho kimeshindwa kupeleka maoni yake bungeni kuhusu miswada ya sheria mbalimbali. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dar es Salaam … (endelea).
Akizungumza katika mdahalo wa wagombea urais wa TLS, uliofanyika leo Jumatano, tarehe 27 Aprili 2022, jijini Dar es Salaam, Sungusia amedai aliwahi kupigiwa simu na maafisa wa Bunge, ambao walimuuliza kwa nini chama hicho hakijapeleka maoni.
“Wakati napigiwa simu na maofisa wa bunge, jamani hatuoni TLS bungeni kuleta maoni kwenye miswada, nilishtuka sana kwamba hata Bunge lilizoea kuona kamati ya katiba ya TLS bungeni kupeleka maoni, haipo bungeni, nilishtuka nikasema some thing not ok,” amedai Sungusia.
Sungusia amedai, TLS haikuitisha kikao cha dharura cha mawakili kwa ajili ya kujadili mchakato wa upatikanaji wa katiba mpya, badala yake kamati yake imewasilisha maoni ambayo amedai siyo msimamo wanachama wake.
“Nikauliza swali TLS imeitisha kikao cha dharura cha mawakili kuhusu hiyo hoja kubwa, nikaambiwa hakuna kikao kilichoitishwa, nikaambiwa ile kamati imefikisha maoni kwa rais, kwamba mchakato wa katiba uje miaka mitano, nikasema huo ndiyo msimamo wetu TLS?” amesema Sungusia.
Sungusia amesema “nikaanza kuona kuna mambo ambayo pengine ninaweza kusaidia na wanachama wenzangu tukasongesha chama cheu mbele.”
Sungusia amesema, endapo atachaguliwa kuwa Rais wa TLS, atarudisha mchango wa chama hicho katika masuala yanayogusa maslahi ya nchi.
“Nataka kurudisha ile relevance ya TLS, mara nyingine watu wanauliza TLS iko wapi? wakili amekamtwa TLS iko wapi? Ninahitaji kuona TLS ambayo ni relevance na inapokuja ajenda ya kitaifa mfano katiba, lazima relevance ya TLS iweze kuonekana,”amesema Sungusia.
Mbali na Sungusia, wagombea wengine katika uchaguzi huo ni, Rais wa TLS anayemaliza muda wake, Profesa Edward Hoseah na Jeremiah Mtobesya.
Leave a comment