FREDERICK Sumaye, aliyekuwa Mwenyekiti wa Chadema Kanda ya Pwani, amelalamika kutoelezwa ‘ukweli,’ kwamba uchaguzi wa ngazi ya uenyekiti kwenye chama hicho, haufuati Katiba ya chama. Anaripoti Regina Mkonde … (endelea).
Akitangaza kujiondoa kwenye chama hicho leo tarehe 4 Desemba 2019, Sumaye amesema hakujua kuwa nafasi ya uenyekiti ndani ya chama hicho ‘ina mwenyewe.’
“Basi wangenitahadharisha katika chama chetu, utaratibu wa uenyekiti uko nje ya Katiba, ningeelewa,” amesema Sumaye.
Amesema, kilichomuondoa Chadema ni ukosefu wa demokrasia “ni pamoja na kufanyiwa figisu kufuatia hatua yangu ya kutangaza kugombea uenyekiti wa chama hiki.”
Amesema, kujitosa kwake kugombea uenyekiti, kulizua nongwa n ahata kufedheheshwa kwenye uchaguzi wa Kanda ya Pwani, kutokana na mkakati uliopangwa.
“Kwa kitendo hiki kilichotengenezwa na wenzangu wa Chadema, nimefedheheka sana, hasa kwa kuonekana nimekosa adabu kwa kutaka kugombea uenyekiti wa Chadema,” ameeleza Sumaye.
Ameeleza kuwa, aliamua kugombea uenyekiti ili kuondoa dhana ya kwamba ndani ya Chadema hakuna demokrasia, na pia nafasi ya uenyekiti wa chama hicho ni ya Mbowe, ambayo haitakiwi kuguswa na mtu yeyote.
“Nongwa ilikuja baada ya mimi kutaka kugombea nafasi ya uenyekiti wa chama chetu. Lengo nilitaka kuondoa hisia iliyojengeka kwenye jamii kwamba ndani ya Chadema hakuna demokrasia ya kweli. Nafasi ya uenyekiti wa Chadema ni ya Mbowe haiguswi na mtu yeyote,” amesema.
Leave a comment