FREDERICK Sumaye, Waziri Mkuu Mstaafu wa Tanzania ambaye aliwahi kuwa Mwenyekiti wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), Kanda ya Pwani amedai, wapo wagombea wanaotaka ‘kuitikisa amani ya nchi.’ Anaripoti Mwandishi Wetu, Dar es Salaam … (endelea).
Amesema, vyama vyenye wagombea hao vinapaswa kuwadhibiti na kwamba, iwapo watashindwa kufanya hivyo, serikali ‘ifanye kazi yake.’
Akizungumza kwenye mahojiano na gazeti moja nchini tarehe 11 Septemba 2020, Sumaye aliyeishi na Chadema kwa miezi 56 kisha kurejea CCM amesema, wagombea hao (bila kutaja majina yao), wamekuwa wakitoa kauli za uchochezi zinazohatarisha amani ya nchi.
“Hao wanaotaka kuleta vurugu, vyama vyao kwanza vingeanza kuwashuhulikia na vikishindwa serikali ipo, iwashughulikia, hatutaki watu wanaoleta fujo kwenye nchi kwa sababu tu wanataka madaraka,” amesema Sumaye.

Amesema, amani ya Tanzania inapaswa kudumishwa kwa kiwango chochote hivyo, mgombea ama viongozi wanaotoa kauli zinazoashirika kuvunjika kwa amani ‘wasivumiliwe.’
Amesema, katika Ukanda wa Afrika, Tanzania ndio nchi pekee wananchi wake wanafurahia matunda ya amani, akisisitiza kuwa “amani si kitu cha kuchezea.”
Sumaye alitangaza kujiunga na Chadema tarehe 22 Septemba 2015, akieleza kwamba alilenga kuimarisha upinzani.
Hata hivyo, tarehe 10 Februari 2020 aliporejea CCM alisema, kwenye vyama vya upinzani hakuna dhamira njema.
“Nilikwenda kujenga upinzani ila kwa nilichokikuta huko, kazi kubwa ni kupamana na polisi na usalama wa Taifa, hawana ajenda nyingine. Hakuna upinzani dhahiri, ni upinzani maslahi,” alisema Sumaye.
Leave a comment