MBUNGE wa Buyungu, Mwalimu, Bilago Kasuku (Chadema) ameibana serikali na kuitaka ieleze ni kifungo gani cha sheria kinaipaMamlaka ya Usimamizi wa Usafiri wa Ardhini na Majini (Sumatra) kutoza ushuru kwa wavuvi na wakati huo huo haifanyi hivyo kwa matrekta ya kilimo, anaandika Dany Tibason.
“Je, Serikali haioni kuwa inadidimiza wavuvi kwa kuwarundikia tozo nyingi na kuwafanya waendelee kuwa Maskini?’’ amehoji Kasuku.
Mwalimu Bilago alitoa kauli hiyo leo bungeni alipokuwa akiuliza swali na nyongeza kwa kuitaka serikali ieleze kama Sumatra kufanya hivyo siyo kudidimiza juhudi za wavuvi.
Akiuliza swali la msingi kwa niaba ya mbunge wa Kigoma Mjini, Zitto Kabwe (ACT Wazalendo) amehoji kuhusina na Sumatra kutoa vibali vya usafiri kwa wavuvi wa Ziwa Tanganyika.
Akijibu swali hilo, Naibu Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, Mhandisi Edwin Ngonyani amesema Sumatra hatoi vibali wala haitozi ushuru kwa vyombo vya usafiri majini nchini ikiwa ni pamoja na wavuvi wa Ziwa Tanganyika.
Ngonyani amesema Sumatra inalo jukumu la kukagua ubora wa vyombo vya usafiri majini ikiwa ni pamoja na vya uvuvi na kutoa cheti cha ubora.
“Moja ya majukumu ya msingi ya Sumatra katika vyombo vya usafiri na vya uvuni ni kuhakikisha vyombo hivyo ni salama kabla ya kuanza kufanya shughuli za majini,’’ amesema.
Amesema mamlaka hiyo inapokagua vyombo vya usafiri majini kwa mujibu wa sehemu ya 11 kanuni ya 9 ya kanuni za sheria ambapo wenye vyombo vya usafiri ikiwa ni pamoja na vya uvuvi.
Kutokana na hali hiyo, Ngonyani amesema serikali haikusudii kudidimiza wavuvi wala haijawarundikia tozo nyingi ambazo ambazo zitawafanya wawe maskini bali inawahakikishia mazingira salama kwa ajili ya kufanya shighuli zao za uvuvi.
Leave a comment