SHIRIKA la Uzashaji Mali la Jeshi la Kujenga Taifa SUMAJKT imekabidhi jozi 500 za viatu vya wanafunzi kwa ajili ya kusaidia kampeni ya Samia Nivishe Viatu. Anaripoti Faki Sosi , Dar es Salaam … (endelea).
Kampeni hiyo inayoongozwa na Msanii Steve Mengele maarufu kama Steve Nyerere, inalenga kutoa msaada wa viatu kwa wanafunzi wasiojiweza kiuchumi vijijini.
Akizungumza na waandishi wa Habari wakati wa makabidhiano ya viatu hivyo Mkurugenzi Mwendeshaji wa Kiwanda cha bidhaa za Ngozi cha Shirika hilo, Meja Mathias Peter, amesema kuwa wameguswa na kampeni hiyo ya kizalendo na kwamba wameamua kutoa juzi hizo ili kuunga mkono kampeni hiyo.
“Sisi kama wazalishaji na watengenezaji wa viatu tuliona jitihada za wenzetu za kuwavisha watoto masikini walioko vijijini, tukaona tuweke mkono hapo kuwapa tabasamu watoto hivyo tunawaunga mkono ndugu zetu hawa kupitia kampeni yao ya Samia Nivishe viatu,” amesema Meja Peter.
Amesema kuwa watoto masikini wanauhitaji wa viatu huko vijijini hivyo shirika hilo limeona kuwa ni uzalendo kuunga mkono kampeni hiyo.
Amesema kuwa katika awamu hii ya kampeni hiyo viatu hivyo vitakwenda kwenye vijiji 6 vya mikoa ya Lindi na Mtwara.
“Kampeni ya Samia Nivishe Viatu ikitekelezwa vizuri itawapa tabasamu watoto masikini ambao hawamudu kununua viatu na utaacha alama kwa watoto hawa,”amesema Meja Peter.
“Sisi SumaJKT ni nyumba ya bidhaa bora vinavyofaa kwa Watanzania mpaka nje ya nchi,” amehitimisha Meja Peter.
Kwa upande wake Steve Mengele amesema kuwa Shirika hilo limeonyesha uzalendo wa hali ya juu kwa kuwaunga mkono ili kuwasaidia watoto masikini.
“Mmeonyesha uzalendo kwa Taifa lakini pia mmefungua milango kuna watu wanaamini kuwa Viatu vya JKT ni kwa ajili ya wanajeshi tu lakini leo hii tumefunguliwa milango kwa raia kuamini kuwa bidhaa zenu kwa ajili ya watu wote,” amesema.
Amesema kuwa wazazi wa wanafunzi wa vijijini hawamudu kuwanunulia watoto wao viatu na kusababisha wanafunzi hao kushindwa kufanya vizuri kwa kuathirika kisaikolojia kwa kokosa viatu.
“Ikienda kule kijijini utamkuta mtoto hajavaa kiatu tangu alipoanza darasa la kwanza mpaka darasa la saba ni ngumu kufanya vizuri kwa kuwa anakwenda shuleni anachomwa na jua anachomwa na miiba tunawashukuru SUMA JKT kwa kutuunga mkono,” amesema Mengele.

Amesema kuwa ubora wa viatu vya Shirika hilo vitawafanya wanafunzi hao wavivae kwa muda mrefu na kumpa uhakika mzazi na kupata nafasi ya kutafuta mahitaji mengine.
Steve amesema kuwa kampeni hiyo imeanza na kugawa viatu kwenye shule za wilaya ya Kibiti na za Mkoa wa Tabora.
Kampuni ya viatu ya SUMAJKT imeanzishwa tarehe 13 Julai 2017, ambapo ina uwezo wa kutengeneza jozi 500 za viatu kila siku .
Inatengeneza bidhaa sita kwa kutumia ngozi kama vile:- Viatu vya Kijeshi, Mikoba ya Pisto, Mikoba ya Wanawake, Viatu vya kiraia aina zote, viatu vya wanafunzi , viatu vya ngozi vilivyochanganywa na kitambaa kigumu, Viatu vya Usalama mahala pa kazi, na Mikanda ya Ngozi.
Leave a comment