MJUMBE wa Kamati Kuu ya Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), Joseph Mbilinyi ‘Sugu’, ameshauri baadhi ya wateule wa aliyekuwa Rais wa Awamu ya Tano, Hayati Dk. John Magufuli, wanaotuhumiwa kwa ufisadi, wachunguzwe ili mali walizojilimbikizia zirudishwe serikalini. Anaripoti Mwandishi Wetu, Arusha … (endelea).
Sugu ametoa wito huo jana tarehe 1 Machi 2023, akizungumza katika mkutano wa hadhara wa Chadema, uliofanyika jijini Arusha.
Mwanasiasa huyo aliyekuwa Mbunge wa Mbeya Mjini kupitia Chadema, alidai kuna baadhi ya waliokuwa mawaziri, wakuu wa mikoa na wilaya katika uongozi wa awamu hiyo, walikuwa wanafanya ufisadi.
“Wanasema awamu ya tano ilizuia ufisadi lakini hakuna awamu iliyokuwa na ufisadi kwa wazi mpaka ngazi ya wakuu wa mikoa kama awamu ya Magufuli na walikuwa wana ukwasi wa hali ya juu, wananyang’anya mali za watu wanajenga nyumba, wanafanya kila kitu wakati mishahara yao ilikuwa Sh. 2 milioni,” alidai Sugu.
Sugu alidai “watu walifanya ufisadi sana haina namna wanatakiwa wachunguzwe ili mali walizoiba kwa umma zirudi kwa wananchi.
Katika hatua nyingine, Sugu amemtaka mrithi wake katika Jimbo la Mbeya Mjini, ambaye ni Spika wa Bunge, Dk. Tulia Ackson, ajiandae kung’oka katika uchaguzi mkuu ujao wa 2025.
“Hii ni salamu kwamba sababu ya mwendazake ndiyo imekuwa hivi, bila mwendazake sio yeye wala dada ake wa Mbeya watakaokwenda kutoboa. Hata uchaguzi ukifanyika kesho asubuhi hawawezi kutoboa,” alisema Sugu.
Leave a comment