POLISI mjini Mombasa nchini Kenya inamtafuta baba mmoja (40) anayetuhumiwa kuchoma moto nyumba ya mpenzi wake iliyoko maeneo ya Magongo, kutokana na wivu wa mapenzi. Anaripoti Regina Mkonde … (endelea).
Baba huyo anayekadiriwa kuwa na umri mkubwa kuliko mpenzi wake ‘Sugar Dady’, anatuhumiwa kufanya tukio hilo usiku wa Jumanne ya tarehe 16 Oktoba 2018 baada ya kukumta mwanamke wake anamsaliti na mwanaume mwengine.
Baada ya kubaini usaliti huo, mtuhumiwa huyo anadaiwa kuchoma moto nyumba ya mwanamke huyo kwa hasira ambao ulisambaa katika nyumba nyingine 11 na kuharibu vitu vyenye thamani ya mamilioni.
Baada ya tukio hilo kutokea, mwanamke huyo anayetuhumiwa kuwa katika mahusiano na wanaume wawili kwa wakati mmoja alichukuliwa maelezo katika Kituo cha Polisi cha Changamwe.
Jirani wa mwanamke huyo, Hamisi Kaju akielezea kuhusu tukio hilo amesema ‘Sugar Dady’ huyo alianza kuchoma moto godoro la mpenzi wake kisha moto kuunguza nyumba nzima na kuenea katika nyumba za jirani.
Shuhuda huyo anadai kuwa, lengo la mwanaume huyo ni kuwadhuru wawili hao aliowafumania ingawa hakufanikiwa.
Leave a comment