MKURUGENZI wa Jiji la Dodoma, Joseph Mafuru amesema wanatarajia kuifumua stendi ya daladala na soko la sabasaba iliyopo katikati ya jiji hilo na kuijenga upya. Anaripoti Danson Kaijage, Dodoma … (endelea)
Hatua hiyo imelenga kuboresha mazingira ya jiji la Dodoma, maeneo ya masoko na stendi ya daladala.
Mafuru ametoa taarifa hiyo leo tarehe 26 Januari, 2022 katika kikao cha baraza la madiwani nijini Dodoma.
Amesema kuwa pamoja na kuwepo kwa changamoto ya masoko na stendi ya daladala, tayari wameanaza kukusanya maoni kutoka kwa wadau ili kuona namna ya kuboresha stendi hiyo, masoko ya sabasaba, majengo na makole.
Amesema stendi ya sabasaba siyo stendi rasmi hivyo kunahitajika uboreshaji mkubwa kwa kufumua stendi pamoja sehemu za biashara.
“Mradi huo unatarajiwa kuanza kati ya Julai na Septemba kwa ufadhili wa Benki ya Dunia na mradi huo mkubwa utakamilika kwa miaka mitatu,” amesema Mafuru.
Katika hatua nyingine amesema jiji la Dodoma ni kati ya majiji ambayo yamepangwa kwa mpangilio mzuri hivyo utaratibu huo utaendelea kutekelezeka.
Aidha, Mafuru amewataka watu wanaoendeleza maeneo yao kufuata utaratibu wa kuomba vibali rasmi vya ujenzi.
Leave a comment