SPIKA wa Bunge la Tanzania, Dk. Tulia Ackson amesema, atazungumza na Waziri wa Habari, Mawasiliano na Teknolojia ya Habari, Nape Nnauye ili kujadiliana kuhusu kurejeshwa au kutorejeshwa kwa ‘Bunge Live.’ Anaripoti Mwandishi Wetu, Dodoma … (endelea).
Dk. Tulia amesema hayo leo Jumatatu, tarehe 14 Februari 2022 wakati akizungumza na waandishi wa habari ikiwa ni siku chache zimepita tangu alipochaguliwa kuwa Spika wa Bunge akichukua nafasi ya Job Ndugai ambaye alijiuzulu.
Katika mkutano huo na waandishi wa habari pamoja na wahariri wa vyombo mbalimbali uliofanyikia ukumbi wa Pius Msekwa bungeni jijini Dodoma, Dk. Tulia ameulizwa kuhusu mikutano ya Bunge kuoneshwa moja kwa moja kama awali.
Dk. Tulia Ackson leo Jumatatu ameuliza na waandishi ana mpango wa kurejesha Bunge live yeye amejibu “Bunge ni daraja je, una mpango wa kurejesha Bunge Live.”
Akijibu swali hilo, Dk. Tulia amesema, “hili ni jambo ambalo linazungumzika na wacha tuone sababu zilizolifanya liwepo na sasa lisiwepo na tutazungumza na waziri wa habari halafu tuone namna ya kulifanyia kazi.”
Amewaomba waandishi wa habari kutoa mawazo, kwani wakati mwingine Bunge kuwa live ni hoja nzuri, lakini lazima utizame ni kitu gani kinakwenda live kwa hao wananchi.
“Si kila kitu utahitaji kuripoti na tutafanya kazi kwa pamoja ili kuona tunalifanyaje jambo hili.
Bunge ‘live’ lilisitishwa Januari mwaka 2016 ikiwa ni miezi kadhaa tangu Serikali ya awamu ya tano iliyokuwa chini ya Rais John Pombe Magufuli (sasa ni marehemu), ilipoingia madarakani tarehe 5 Novemba 2015.
Waziri wa wakati huo wa iliyokuwa wizara ya habari, utamaduni, sanaa na michezo, Nape Nnauye alitoa sababu mbalimbali za kuamua kusitishwa kwa Bunge live ikiwemo gharama kuwa kubwa iliyokuwa inaingia Shirika la Utangazaji Tanzania (TBC) ya zaidi ya Sh.4 bilioni kwa mwaka na nyingine wananchi walikuwa wanashindwa kufanya kazi kisa kufuatilia mikutano ya Bunge.
Kwa sasa Nape ambaye aliondolewa kwenye uwaziri, amerejeshwa kwenye baraza la mawaziri na Rais Samia Suluhu Hassan akitumikia wizara ya habari, mawasiliano na teknolojia ya habari.
Leave a comment