SPIKA wa Bunge, Dk. Tulia Ackson, ameagiza Serikali kuweka kanzi data maalum (data base), yenye taarifa za watumishi wanaojitolea ili wapewe kipaumbele katika mchakato wa ajira. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dodoma … (endelea).
Spika Tulia ametoa agizo hilo leo tarehe 6 Aprili 2023, bungeni jijini Dodoma, baada ya Mbunge Viti Maalum, Felista Njau kuhoji lini Serikali itaajiri watalaamu wanaojitolea kwa muda mrefu kufanya kazi katika sehemu mbalimbali nchini.
“Waziri wa Afya na wa TAMISEMI, nafikiri kuna haja ya kukaa na Ofisi ya Rais Utumishi na Utawala Bora, sababu watumishi wa afya wanaojitolea na walimu wanaojitolea huwa haipendezi sana kuachwa kwenye ajira. Sababu ajira zikitangazwa wale wanaojitolea unajikuta kwenye eneo lako hakuna mmoja aliyepata ajira, tunajiuliza hawana sifa na wanaokaa nyumbani ndiyo wana sifa?” amesema Dk. Tulia na kuongeza:
“Nafikiri mtengeneze utaratibu mzuri ili kila mwaka mpate taarifa za wanaojitolea ili ajira zinapopatikana mzitumie taarifa hizo kuwapa kipaumbele.”
Awali akimjibu Njau, Naibu Waziri wa Afya, Dk. Godwin Mollel, alisema wizara imetoa muongozo wa kuwalipa nusu mshahara watumishi wanaojitolea kwa kutumia mapato ya ndani.
Aidha, Dk. Mollel alisema hospitali za mikoa, kanda na taifa zimeweza kuwalipa mishahara kamili asilimia 40 ya watumishi wanaojitolea , kwa kutumia mapato ya ndani.
Alisema Wizara ya Afya, itashirikiana na Wizara Ofisi ya Rais TAMISEMI, kuangalia namna bora ya kuwapa kipaumbele kwenye ajira watumishi wanaojitolea kuliko waliokuwa nje ya mfumo huo wakisubiri ajira moja kwa moja.
Leave a comment