JOB Ndugai, Spika wa Bunge, amesema akifanya vibaya katika kuungoza mhimili huo, wa kulaumiwa ni Spika Mstaafu, Mama Anna Makinda, aliyekuwa mwalimu wake. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dodoma … (endelea).
Spika Ndugai ametoa kauli hiyo leo Alhamisi, tarehe 10 Juni 2021, alipokuwa anamtambulisha Mama Makinda, aliyehudhuria bungeni jijini Dodoma, kwa ajili ya kusikiliza uwasilishwaji Bajeti Kuu pendekezwa ya Serikali, kwa mwaka wa 2021/22.
Kiongozi huyo wa Bunge amesema, Mama Makinda alimpokea bungeni, ambapo alishirikiana nae kwa karibu, katika nafasi mbalimbali za uongozi alizopitia bungeni.
“Nimtambulishe Spika Mstaafu Makinda, mama alikaa bungeni takribani miaka 40, ni rekodi ambayo sio rahisi. Hata nyie wabunge mnasema vijana, naye alikuja kama kijana. Miaka 40 aliyokaa humu ni shughuli kubwa,” amesema Spika Ndugai.
Akielezea historia yake na Mama Makinda, Spika Ndugai amesema, alipoingia bungeni kwa mara ya kwanza 2000, kupitia Jimbo la Kongwa, mkoani Dodoma, alipangwa kwenye Kamati ya Ardhi, Maliasili na Mazingira, ambapo mwanasiasa huyo alikuwa Mwenyekiti wake.
Spika Ndugai amesema, miaka mitano baadae, Mama Makinda alikuwa Mwenyekiti wa Bunge, huku yeye akichukua nafasi yake ya uenyekiti wa Kamati ya Ardhi, Maliasili na Mazingira.
Mwanasiasa huyo amesema, baadae (2005 hadi 2010) alichaguliwa kuwa Mwenyekiti wa Bunge, huku Mama Makinda akiwa Naibu Spika wa Bunge. Nafasi aliyokuja kumrithi baada ya mwanamama huyo kuchaguliwa kuwa Spika wa Bunge.
Spika Ndugai alikuwa Naibu Spika wa Bunge, kuanzia 2010 hadi 2015.
Baada ya Mama Makinda kustaafu Uspika wa Bunge 2015, Spika Ndugai alimrithi katika nafasi hiyo.
“Ameenda kustaafu nimekuwa spika, kwa hiyo mie huwa nafuata mguu wake, anapotoa naweka. Kwa kuwa amestaafu na mimi nafuatia futia, nitawaambia hapo mbele, bado kazi yangu kufuata nyayo zake,” amesema Spika Ndugai na kuongeza:
“Namshukuru sana mama kwa malezi, mkiona naharibu kwa kweli alaumiwe yeye maana yeye ni mwalimu wangu kila hatua.”
Leave a comment