JOB Ndugai, Spika wa Bunge la Jamhuri amesema, Tundu Lissu, aliyekuwa Mbunge wa Singida Mashariki amejitajia mwenyewe ‘kuvuliwa ubunge.’ Anaripoti Danson Kaijage, Dodoma…(endelea).
“Kwa maoni yangu hili ni la kujitakia tu kama lile la Arumeru Mashariki (Joshua Nassari), wewe unakaa karibu mwaka huwasiliani chochote, na hata chama chako hakikuwahi kuniambia, na hata kiongozi wa upinzani hajawahi kuniambia,” amesema Spika Ndugai.
Spika Ndugai ametoa kauli hiyo leo tarehe 9 Septemba 2019, baada ya Mahakam Kuu Kanda ya Dar es Salaam kutupilia mbali maombi ya Lissu ya kuvuliwa ubunge wake.
Akizungumza bungeni jijini Dodoma amesema, uamuzi huo wa mahakama haukumuonea mtu kwa kuwa Lissu alishindwa kuheshimu mamlaka ya Bunge.
“Mambo mengine haya mtayasikia wenyewe huko nje mtakapotoka, sitaki kuyasema. Si ndio leo tarehe 9 bwana? au leo tarehe ngapi? mambo haya, ukiheshimu mamlaka ukashirikiana na mamlaka huwezi kupata matatizo haya,” amesema Spika Ndugai.
Spika Ndugai amedai kuwa, kitendo cha Lissu kutompa taarifa ya udhuru katika mikutano ya bunge kwa sababu ya kuumwa, huku akionekana kufanya shughuli nyingine ni kukiuka taratibu za mhimili huo.
“Bunge kama hili linaloendelea, wewe uwe unaumwa lakini sio kwamba uko mahututi kiasi hicho hivi kumjulisha spika tu, mimi siwezi kuhudhuria bunge, kwasababu kama unavyojua niko hospitali naendelea na matibabu, bado naumwa na kikaratasi cha daktari wako unakibandika pale unanitumia, kuna ubaya gani?” amehoji Spika na kuongeza;
“Kwa hiyo, mengine yote unafanya isipokuwa kumwambia spika? Mwaka unapita nakuona tu huko wapi, mengine yote unaweza kufanya lakini kuwasiliana na huyu hufanyi. Haiwezekani, itafika mahali watu wataruka na wewe tu na usipige kelele, umeyataka mwenyewe sababu taratibu uanzijua.”
Aidha, Spika Ndugai amesema, hatokuwa na ugomvi na mtu anayefuata taratibu za Bunge.
“Ukifuata taratibu hatuna ugomvi, habari ya fomu za maadili lazima tujaze ni takwa la katiba, hata Freema Mbowe alipokuwa magereza aliniandikia barua Disemba iliyopita kuwa, niko mahali ambako siwezi kujaza fomu Segerea lakini nikitoka nitajaza, kulikuwa na ugomvi? alivyotoka alijaza,” amesema Spika Ndugai.
Mahakama Kuu Kanda ya Dar es Salaam mbele ya Jaji Sirillius Matupa, leo imetupilia mbali ombi la Lissu la kupinga uamuzi wa bunge kumvua ubunge wa Singida Mashariki, kwa hoja ya kwamba lingeweza kuleta mgogoro wa kikatiba.
Katika ombi lake hilo, Lissu aliieleza mahakama hiyo kwamba uamuzi wa kumvua ubunge haukuwa sahihi kwa kuwa alihukumiwa bila ya kupewa nafasi ya kujieleza, juu ya makosa aliyotuhumiwa kufanya yaliyopelekea bunge kuchukua uamuzi huo.
Lissu alivuliwa ubunge tarehe 28 Juni 2019 na taarifa ya uamuzi huo ilitolewa bungeni na Spika Ndugai, aliyeeleza sababu mbili za mhimili huo kuchukua hatua hiyo ikiwemo, mwanasiasa huyo kutohudhuria vikao vya bunge bila taarifa na kutojaza fomu ya maadili.
Kwa sasa jimbo la Singida Mashariki linashikiliwa na Miraji Mtaturu wa Chama cha Mapinduzi (CCM). Mtatura ameapishwa bungeni tarehe 3 Septemba mwaka huu.
Leave a comment