JOB Ndugai, Spika wa Bunge ametumia ujio wa Mukabalisa Donatile, Spika wa Bunge la Rwanda kuwanaga wapinzani nchini. Anaripoti Regina Mkonde…(endelea).
Spika Ndugai akizungumza bungeni jijini Dodoma wakati wa kumtambulisha Spika Donatile leo tarehe 10 Juni 2019 amesema, wapinzani wa Rwanda hapingi kila kitu kama walivyo wapinzani wa Tanzania.
Spika Ndugai amesema, Rwanda iko tofauti na Tanzania kutokana na kuwa na vyama vya ushindani na si vya kupinga kila kitu.
“Tofauti na hapa kwetu ni kwamba, Spika wa Rwanda kwenye Katiba yao anatoka chama tofauti na tawala, lakini niseme kwamba Rwanda hawana vyama pinzani vya kupinga kila kitu kama hapa.
“Wao wana vyama ushindani tofauti kubwa ni hapo, kile cha kupinga na kubisha haiwezekani,” amesema Spika Ndugai.
Spika Donatile aliwasilisi nchini jana tarehe 9 Juni 2019 kwa ziara ya kikazi ya siku tatu, ikiwemo kukutana na wabunge, kamati mbalimbali za Bunge, Chama cha Wabunge Wanawake (TGWP).
Pia, atafanya ziara katika maeneo mbalimbali jijini Dodoma na kumtembelea Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa na Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Prof. Palamagamba Kabudi.
Leave a comment