KUFUATIA kifo cha Rais wa Tanzania, Dk. John Magufuli, kilichotokea tarehe 17 Machi 2021 katika Hospitali ya Mzena jijini Dar es Salaam, Spika wa Bunge, Job Ndugai amesitisha ziara za kamati za mhimili huo za kukagua miradi mbalimbali. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dodoma…(endelea).
Agizo hilo la Spika Ndugai limetolewa leo Alhamisi tarehe 18 Machi 2021, baada ya kifo cha Rais Magufuli kutangazwa na Makamu wa Rais, Samia Suluhu Hassani.
Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa na Ofisi ya Spika, Spika Ndugai amewaagiza wajumbe wa kamati hizo kurejea mara moja katika Makao Makuu ya Nchi, Dodoma.
“Kufuatia msiba huu mkubwa, Mheshimiwa Spika ameagiza kamati zote za Bunge zilizokuwa katika ziara za ukaguzi wa miradi ya maendeleo mikoani, kurejea Dodoma mara moja,” imesema taarifa ya Ofisi ya Spika.
Akielezea kifo cha Rais Magufuli, Spika Ndugai amesema msiba huo ni mzito ambapo ametoa pole kwa mke wa marehemu, Mama Janeth Magufuli, familia yake, Mama Samia na Watanzania kwa ujumla.
“Tumempoteza Rais wetu kipenzi aliyejitoa kuwatumikia Watanzania wote kwa uadilifu, umahiri, bidii na moyo wa uzalendo wa hali ya juu.
“Kwa niaba ya Bunge, natoa pole kwa Mama Janeth Magufuli na familia ya marehemu, Makamu wa Rais pamoja na Watanzania wote kufuatia msiba huu mzito wa kitaifa,” amesema Spika Ndugai.
Leave a comment