LICHA ya Kamati Kuu ya Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema) nchini Tanzania, kuwavua uanachama wabunge wake wanne, kwa kutotii maagizo ya chama hicho, Spika wa Bunge nchini humo, Job Ndugai amewakingia kifua wabunge hao. Anaripoti Regina Mkonde…(endelea).
Jana Jumatatu, tarehe 11 Mei 2020, John Mnyika, Katibu Mkuu wa Chadema, alitangaza maazimio ya kikao cha kamati kuu kilichokutana kwa njia ya kidijitali tarehe 9 na 10 Mei 2020 chini ya Mwenyekiti wake, Freeman Mbowe na kuridhia adhabu mbalimbali kwa wabunge wake.
Wabunge waliovuliwa uanachama na majimbo yao kwenye mabano ni, Anthony Komu (Moshi Vijijini), Joseph Selasini (Rombo), David Silinde (Momba) na Wilfred Lwakakatare (Bukoba Mjini).
Wakati wabunge hao wane wakivuliwa ubunge, wengine 11 wametakiwa kujieleza kwa nini wasichukuliwe hatua za kinidhamu.
Wabunge hao ni; Susan Maselle , Joyce Sokombi, Rose Kamili, Latifa Chande, Lucy Mlowe, Lucia Mlowe, Lucy Magereli na Dk Sware Semesi (wote Viti Maalumu).
Wengine ni; Willy Qambalo (Karatu), Peter Lijualikali (Kilombero) na Japhary Michael (Moshi Mjini).
Mnyika alisema kamati hiyo imefikia uamuzi huo, baada ya wabunge hao kukiuka maagizo ya Chadema ya kutohudhuria bungeni kwa muda wa siku 14, kwa ajili ya kujiweka karantini kuangalia kama wa maambukizo ya virusi corona (Covid-19).
Hata hivyo, wabunge hao 15 wakiwamo waliofukuzwa walikaidi maagizo hayo na kuamua kuhudhuria shughuli za Bunge linaloendelea jijini Dodoma la kujadili bajeti ya Serikali ya mwaka 2020/21.
Spika Ndugai akiahirisha shughuli za Bunge jana Jumatatu jioni tarehe 11 Mei 2020 alizungumzia uamuzi huo wa Chadema akisema atawalinda wabunge hao kwani hakuna jambo walilofanya lililoenda kinyume na sheria za nchi.
“Lakini niseme tu kwamba wabunge mnaapishwa na spika, na karibu wote nimewaapisha mimi mwenyewe hapa. Sasa wabunge wangu niliowaapisha wala msiwe na wasiwasi . Hakuna cha nini wala nini, vikao vya majungu hivyo yaani havifanyi kazi,” alisema Spika Ndugai
“Endeleeni kuhudhuria wala msiwe na mashaka, tutawalinda kwa kuwa hakuna jambo lolote ambalo mnalofanya kinyume na sheria.”
Spika Ndugai amesema atawalinda wabunge hao kwa kuwa walichaguliwa na wananchi, hivyo mtu mmoja hawezi kuwa na mamlaka ya kuwafukuza kwa kuwa wameshindwa kufanya anavyotaka.
“Eti mtu mmoja katika nchi hii anajifanya yeye ana mamlaka ya kufukuza wabaunge anavyotaka, hiyo haiwezekani, hiyo biashara itashia huko huko. Lakini sio Tanzania hii, huwezi kujenga ufalme wa aina hiyo,” alisema Spika Ndugai.
Spika Ndugai alihoji, “Mbunge akipata mashahara lete huku sehemu ya mshahara, yaani wananchi mnachagua mbunge anaenda kuwa mtumwa wa mtu kweli? hata akihudhuria kikao cha bunge kisa yeye hataki basi adhabu yake kufukuzwa, hilo jambo halipo.”
Kiongozi huyo wa Bunge alitumia fursa hiyo kushauri Ofisi ya Msajili wa Vyama vya Siasa, kuifuatilia Chadema pamoja na vyama vingine .
“Na msajili hebu aangalie vyama vya namna hii. Na kwa dalili hizi, sijui sababu anaona yeye mwenyewe Novemba harudi, hapa sasa anaharibia wenzake mambo magumu haya,” alisema Spika Ndugai.
Katika hatua nyingine, Spika Ndugai alisema msimamo wake wa kuwakata fedha wabunge wasiohudhuria vikao vya bunge, uko pale pale, huku akiwataka pindi watakaporejea bungeni, waje na cheti kinachoonyesha matokeo ya kipimo cha Covid-19.
“Kesho (leo) tutatoa orodha, maana tunapiga mstari wa wale wasio tii maelekezo ya kiti mpaka sasa. Maelekezo yale bado yako pale pale kurudisha hizo fedha. Kwa wale ambao hawajatii na watakapokuja lazima kila mmoja aje na cheti ya kuwa umepimwa Covid-19 na ameonekana hauna, vinginevyo hautapokelewa,” alisema Spika Ndugai.
Leave a comment