SPIKA wa Bunge la Tanzania, Job Ndugai ameishauri Wizara ya Fedha na Mipango, iache kuchukua fedha za miradi ya maendeleo, za halmashauri zinazochelewa kuzifanyia kazi kutokana na sababu mbalimbali. Anaripoti Jemima Samwel, DMC … (endelea).
Spika Ndugai ametoa ushauri huo leo Jumanne tarehe 25 Mei 2021, bungeni jijini Dodoma, baada ya Mbunge Viti Maalum, Christina Mnzava, kuhoji lini Serikali itarejesha fedha za ujenzi wa Hospitali ya Halmashauri ya Msalala, zilizorudishwa na mfumo baada ya mwaka wa fedha wa 2019/2020, kuisha.
Kiongozi huyo wa Bunge, ameitaka wizara hiyo iliangalie kwa makini suala la fedha za miradi ya maendeleo zilizochelewa kutumika, kurudishwa Serikalini baada ya mwaka wa fedha kuisha.
“Serikali inabidi mliangalie hili, mwezi huu wa tano unapeleka Sh. 1 bilioni kwa ajili ya ujenzi wa shule ya sekondari. Unajua kuna mambo ya manunuzi, halafu unataka mkurugenzi wa Ngara akuandikie barua hazina kukwamibia siwezi kuzitumia,” amesema Spika Ndugai.
Spika Ndugai amesema “yaani wewe unayepeleka hela huoni mwezi wa tano unaisha, ukijua tarehe 15 Juni unazichukua hela zilezile, sio sawa. Yeye mwenyewe anapaswa kujua hizi hela nilizopeleka ni za miradi. Mliangalie hilo, Serikali kuchukua hela kwa wananchi siyo sawa.”
Spika Ndugai amesema kitendo cha fedha hizo kuchukuliwa, kinaawaathiri wananchi.
“Huu utaratibu wa kuchukua fedha, unachukua kwa ajili gani? Kwa nini unachukua wakati hela ni za mradi? Anayeathirika ni mwananchi siyo mkurugenzi,” amesema Spika Ndugai na kuongeza:
“Wizara ya Fedha waangalie, haya ni masuala ya maendeleo ya wananchi, siyo tu chukua lete. Tena wanachukua kwenye mfumo, hakuna mwenye taarifa manshtukia tu sifuri kwenye akaunti. Naomba hilo mliangalie.”
Awali, Naibu Waziri Ofisi ya Rais-Tamisemi, Dk. Festo Dugange, alisema mifumo inayopeleka fedha za miradi ya maendeleo katika halmashauri, kutoka Wizara ya Fedha ina mapungufu.
“Spika mifumo ambayo kimsingi inatumika katika kupeleka hizi fedha na kutumia, zina changamoto zake, lakini Serikali inaendelea kuboresha kuhakikisha wishoni mwa mwaka, inafanya kazi kuhakikisha miradi ya mendeleo inaendelea kutekelezwa,” alisema Dk. Dugange.
Aidha, Dk. Dugange amewashauri wakurugenzi wa halmashauri nchini, ambao wanashindwa kuzitumia fedha hizo kwa wakati, kuandika barua ya kuomba kibali maalum cha matumizi ya fedha hizo.
“Sheria ya Bajeti namba 11 ya mwaka 2015, inaeleza vizuri utataratibu wa fedha zinazopelekwa kwenye Mamlaka ya Serikali za Mitaa, ambazo zimepelekwa malengo mahsusi lakini hazitatumika mpaka tarehe 30 Juni kwa mwaka husika wa fedha,” amesema Dk. Dugange.
Naibu Waziri huyo wa Tamisemi amesema “Utaratibu uliolekezwa kisheria ni kwamba, wakurugenzi wakishaona fedha zimeingia kwa kuchelewa na kwa mazingira halisi hawawezi kutekeleza majukumu yake kwa wakati.”
“Wanatakiwa kuandika barua kwa katibu mkuu hazina, kupitia katibu mkuu Tamsiemi, kuomba maombi maalum na kutoa sababau za msingi kwamba fedha zile hazitaweza kutumika kwa terehe husika . Na hivyo wapewe kibali maalum cha kutumia fedha zile ndani ya robo ya kwanza ya mwaka wa fedha unaofuata,” amesema Dk. Dugange.
Leave a comment