MWENYEKITI wa Serikali ya Kijiji cha Mabuki- Kata ya Mabuki -Halmashauri ya Wilaya ya Misungwi mkoani Mwanza Selemani Masoud amesema kuwa Soko la mazao ya nafaka katika Kijiji hicho halina choo hali ambayo inahatarisha afya za watumiaji wa soko hilo. Anaripoti Paul Kayanda, Misungwi… (endelea).
Hayo yanajiri wakati soko hilo la Mabuki liloanzishwa mwaka 1988, kuwa chanzo cha mapato ya ndani katika Halmashauri hiyo ya Misungwi.
Soko hilo linakusanya wafanyabiashara kutoka maeneo mbalimbali pamoja na umati mkubwa wa wananchi wa vijiji vya kata mbalimbali wilayani hapa wanaokuja kupata huduma ya soko hilo.
Akizungumza na waandishi wa habari mwishoni mwa wiki Mjini hapa, Mwenyekiti wa serikali ya Kijiji hicho, Selemani Masoud soko hilo linanufaisha Halmashauri pamoja lakini wananchi wa kijiji chake na vijiji jirani vya kata za pembezoni wanapatiwa huduma mbovu.
“Sisi kama Kijiji hatunufaiki na hili gulio, Halmashauri wanakuja kukusanya ushuru na hakuna kiasi chochote kinachoachwa kwa ajili ya maendeleo yetu na mpango tulionao sasa kama halmashauri wataendelea kuchelewa tutatafuta wadau wa hapa hapa kijijini ili wajenge tuingie ubia nao wa kukusanya chochote kwa ajili ya Kijiji,” alisema.
Alifafanua kuwa soko hilo lilianzishwa tangu mwaka 1988 mpaka sasa wananchi wanafanya biasahara zao bila choo na kuongeza kuwa wakibanwa haja wanakwenda nyumba za jirani ama vichakani kulingana na jiografia ya eneo lilipo soko hilo.
Hata hivyo, Diwani wa Kata hiyo, Malale Lutonja alikiri kuwepo kwa changamoto hiyo kwa kipindi kirefu na kudai kuwa Halmashauri ipo mbioni kutatua kero hiyo ukilinganisha kuwa soko hilo ni sehemu ya chanzo cha mapato ya ndani.
Leave a comment