NATAMANI Tanzania iliyo tofauti na ya sasa, natamani Tanzania isiyogawika, tena isiyo na fursa ya kuwafanya hawa wawe chini au hawa juu. Tanzania ambayo wananchi wote watatembea kifua mbele. Anaripoti Regina Mkonde, Dar es Salaam … (endelea).
Kauli hiyo ameitoa Lazaro Nyalandu, Mwenyekiti wa Chama Cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema) Kanda ya Kati, wakati akichukua fomu ya kuomba kuteuliwa kugombea Urais wa Tanzania kupitia chama hicho.
Nyalandu amekabidhiwa fomu hiyo leo Jumatano tarehe 8 Julai 2020 na Reginald Munisi, Mkurugenzi wa Uchaguzi Chadema katika Makao Makuu ya chama hicho Kinondoni, jijini Dar es Salaam.
Nyalandu amekuwa mwanachama wa nne kuchukua fomu Chadema. Zoezi hilo linalotarajia kumalizika tarehe 19 Julai 2020. Lilianza tarehe 4 Julai 2020.
Soma zaidi:-
-
Wakili amfuata Lissu urais Chadema
-
Dk. Mayrose achukua fomu ya urais Chadema, aahidi chakula na mishahara bora
-
Lissu achukua fomu ya urais Chadema
Wa kwanza kuchukua fomu hiyo ni Tundu Lissu, aliyechukua fomu Jumamosi tarehe 4 Julai 2020 kupitia wakala wake David Jumbe. Akafuatiwa na Dk. Mayrose Majinge, aliyechukua jana tarehe 7 Julai 2020.
Nyalandu ambaye aliwahi kuwa Waziri wa Maliasili na Utalii katika Serikali ya Awamu ya Nne, amesema atarejesha umoja wa kitaifa na kuondoa tofauti za kisiasa.
“Jambo la kwanza ni kuhakikisha tunarejesha umoja wa kitaifa. Matumaini ya Watanzania ya udugu, upendano na ushirikiano, penye lawama tupeleke upendo.
“Kama mimi nilipokuwa CCM nilimshika mkono Mbowe (Freeman Mbowe) na tukafanya kazi. Umoja ule wa kitaifa upite tofauti zetu tunazoziona,” amesema Nyalandu.
Amesema, anatamani kuiona Tanzania inayoongozwa na Katiba mpya itakayodadavua na kurekebisha mifumo iliyoanza kuyumba, kutokana na baadhi ya watu alioanza kuichakachukua kutokana na udhaifu wa hiyo mifumo.
“Wakati naondoka CCM nilisema, ili nchi iwe sawaswa ni lazima serikali, mahakama na bunge viwe huru. Haya mafiga matatu yanatakiwa yajitegemee na yajiendeshe pamoja,” amesema Nyalandu.
Wakati huo huo, Nyalandu ameahidi kama atafanikiwa kuwa Rais wa Tanzania, ataboresha mifumo ya utoaji haki pia kufuta msemo wa ‘wataisoma namba’ kwa Watanzania.
“Hatutaki Mtanzania aisome namba yoyote zaidi ya namba ya kheri ya Tanzania, tunataka Tanzania yenye Watanzania wenye haki ya kukosoa serikali.
“Serikali yetu wajiandae kukosolewa na wale wanaokosoa warudi nyumbani salama. Hivyo tutandaa Taifa lenye mawazo tofauti yatakayojenga Taifa bora,” amesema Nyalandu.
Tarehe 22 Julai 2020, Kamati Kuu ya Chadema itapendekeza jina la mgombea urais, kisha tarehe 29 Julai 2020, mkutano mkuu wa Chadema utapitisha jina la mgombea wa urais wa Tanzania.
Leave a comment