IGP Simon Sirro, Mkuu wa Jeshi la Polisi nchini amesema, kwenye Uchaguzi Mkuu wa Oktoba 2020, jeshi hilo halitaki matatizo na mtu yeyote. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dar es Salaam … (endelea).
Akizungumza na wanahabari jijini Dar es Salaam amesema, uchaguzi huo anapenda kuona unapita kwa amani na viongozi wa kutumikia taifa hili wanapatika bila vurugu yoyote.
“Tunataka uchaguzi wa mwaka huu uwe wa kuaminika, tunataka uchaguzi ambao ni wa haki kama Rais John Magufuli alivyosema. Hatutaki kufikia mahala kuanza kutoa mabomu ya machozi, sasa hivi tunataka tujipange vizuri, tupate viongozi wetu bila matatizo yoyote,” amesema IGP Sirro.
Pia amewataka wadau wa uchaguzi, ikiwemo wanasiasa na viongozi wa dini, kutekeleza wajibu wao ipasavyo kwa kushirikiana na jeshi hilo, ili uchaguzi huo ufanyike pasi na dosari yoyote.
“Kila mtu kwenye nafasi yake ana kila sababu ya kujua wadau ni watu gani kwenye uchaguzi. Maana yake uchaguzi hauwezi kuwa salama kwa kutegemea Jeshi la Polisi peke yake.
“Kwa hiyo kuna wadau ni lazima washirikiane nao, viongozi wa dini wanasiasa na wananchi wenyewe,” amesema IGP Sirro.
Tayari vyama vya siasa nchini ikiwemo CCM, Chadema, CUF, ACT-Wazalendo vimeanza mchakato kuelekea uchaguzi huo.
Dk. Charles Mahela, Mkurugenzi wa Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC), wakati akizungumza na Mwanahalisi Online hivi karibuni, alisema tume hiyo itaanza kufanya uteuzi wa wagombea, baada ya bunge kuvunjwa, kisha taratibu zingine zitafuatwa.
Leave a comment