WAZIRI wa Mambo ya Ndani ya Nchi, George Simbachawene, amesema Jeshi la Polisi limefanikiwa kudhibiti vitendo vya uhalifu wa kutumia silaha ‘ujambazi’ ulioibuka hivi karibuni. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dar es Salaam…(endelea).
Simbachawene ametoa kauli hiyo jana tarehe 3 Julai 2021, akizungumza na wananchi wa Jimbo lake la Kibakwe, jijini Dodoma.
Simbachawene alisema, jeshi hilo limefanikiwa kuwanyamazisha kimyakimya majambazi katika maeneo mbalimbali nchini, baada ya hivi karibuni kuijaribu Serikali.
Simbachawene alisema baadhi ya matukio ya ujambazi yalitokea hivi karibuni, katika baadhi ya miji ya Dar es Salaam, Arusha na Mwanza.
Waziri huyo wa mambo ya ndani alisema, majambazi hao walinyamazishwa katika operesheni ya kwanza ya kupambana na majambazi, iliyofanyika hivi karibuni nchi nzima.
Huku akiwaonya wahalifu hao wasiendelee kuijaribu Serikali, kwa kuwa inaendelea kufanya operesheni ya awamu ya pili.
“Wapo watu wengine wanafikiri uhalifu utawasaidia, kwa wale ambao wanavichwa vigumu wanaendelea kuichezea Serikali kwa kutokutaka kuacha uhalifu, kuacha ujambazi wa kutumia silaha, wanaopenda kubaka, wanaopenda kunyang’anya, wanaotumia pikipiki kupora,”
“Sisi tumeyaweka makosa hayo kama makosa makubwa, tukikukamata tunamalizana naye kimyakimya, wewe utajua kimyakimya tunamalizana kinamna gani,” alisema Simbachawene.
Simbachawene aliwataka Watanzania kufanya kazi halali, kwa kuwa fursa za kiuchumi zipo nyingi nchini, kuliko kufanya uhalifu ambao utawaletea matatizo.
“Nawaomba Watanzania na leo nazungumzia hapa Lufu, Jimbo la Kibakwe, Wilaya ya Mpwapwa, nataka kauli hii ifike nchi nzima, kwamba uhalifu sio dili,
Serikali ipo makini, tutadili na wahalifu wote mpaka tone la mwisho.
Acheni kufanya uhalifu, ukiwa mtu wa kupanga mambo yako utafanikiwa tu, lakini uhalifu hauwezi kukusaidia,” alisema Simbachawene.
Leave a comment